SERIKALI ya Tanzania imepatiwa msaada wa Sh. 32.74 bilioni kutoka Ujerumani kwa ajili ya kutokomeza vifo vitokanavyo na uzazi, pamoja na kudhibiti maambukizi ya Virusi vya Ukimwi (V.V.U) kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Fedha hizo zimetolewa na Ujerumani kwa ajili ya utekelezaji wa awamu ya tatu ya mradi wa ‘Tumaini la Mama’ unaotoa huduma kwa kina mama na watoto wanaotoka kwenye kaya masikini, unaotekelezwa na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF).
Mkataba wa msaada huo ulisainiwa jana tarehe 9 Septemba 2019 jijini Dar es Salaam na Doto James , Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango pamoja na Dk. Annika Calov, Mkurugenzi wa Benki ya Maendeleo ya Ujerumani.
Akizungumza baada ya kusaini mkataba huo, James amesema sehemu ya fedha hizo zitatumika kununua vifaa tiba vinavyohusiana na afya ya uzazi kwa ajili ya kuimarisha utoaji wa huduma za afya katika mikoa iliyochaguliwa kunufaika na mradi huo.
Dk. Calov amesema fedha hizo zitasaidia kuboresha afya ya mama na mtoto pamoja na kuzia maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda na mtoto katika mikoa ya Mbeya, Songwe, Tanga, Lindi na Mtwara.
Kwa upande wake Bernard Konga, Mkurugenzi Mkuu wa NHIF amesema tangu mradi huo uanze mwaka 2012, kina mama 1,157,191 wamenufaika nao kwa kuwa na bima ya afya kupitia shirika hilo.
Leave a comment