MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kinondoni, jijini Dar es Salaam, imeahirisha kutoa hukumu ya kesi ya kubaka inayomkabili Isack Jacob kutokana na hali ya afya ya mshtakiwa huyo kutokuwa nzuri. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Hukumu hiyo ilipangwa kutolewa leo tarehe 15 Machi 2023 mahakamani hapo mbele ya Hakimu Mkazi, Amos Rweikiza lakini imeahirishwa hadi tarege 28 Machi mwaka huu.
Ni baada ya wakili wa mshtakiwa huyo, Kanti Mjata kudai mahakamani hapo kwamba mteja wake hakufika kortini kutokana na kuumwa.
Wakili Mjata alidai kuwa hivi karibuni mshtakiwa alienda hospitalini kufanyiwa vipimo vya afya na kubainika kuwa mgonjwa.
Wakili Mjata aliomba mahakama iahirishe kusoma hukumu hiyo hadi wakati mwingine atakapoweza kufika mahakamani.
Baada ya ombi hilo, Hakimu Rweikiza aliahirisha kesi hiyo hadi tarehe 28 Machi 2023, ambapo ametoa amri ya mshtakiwa kufika mahakamani siku tajwa ili hukumu dhidi yake iweze kutolewa.
Kesi hiyo ya jinai Na. 281/2020, ilifunguliwa na baba mzazi wa mwanafunzi huyo ambaye jina lake limehifadhiwa, Jonathan Machemba, akimtuhumu kwamba amembaka binti yake.
Anadai kuwa mtuhumiwa alitenda kosa hilo kwa nyakati tofauti akiwa nyumbani kwake maeneo ya Kijitonyama, jijini Dar es Salaam, wakati binti yake akiwa na umri wa miaka 17.
Inadaiwa kuwa, baada ya baba huyo kubaini binti yake amebakwa, alimpeleka katika Hospitali ya Mloganzila, jijini Dar es Salaam, kisha vipimo vya daktari kubaini kuwa aliingiliwa na mwanaume anayedaiwa kuwa Jacob.
Hata hivyo, wakati akijitetea mshtakiwa huyo alidai mahakamani hapo kuwa, hakuwahi kumbaka binti yake Machemba, bali mwanafunzi huyo alikubali kwa hiari yake na kwamba aliwahi kumnunulia simu ya mkononi kama sehemu ya makubaliano yao.
Licha ya utetezi huyo, mwanafunzi huyo alikana taarifa hizo na kudai kwamba mshtakiwa alikuwa anambaka.
Leave a comment