UBALOZI wa Ufansa umefungua ofisi ndogo mkoani Dodoma ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono jitihada zinazaofanywa na Serikali, kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia na mataifa mbalimbali. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dk. Stergomena Tax, akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa ofisi hiyo jijini hapo, amesema tukio hilo ni sehemu ya jitihada zinazofanywa na Serikali katika kuimarisha ushirikiano wa kimataifa.
Dk. Tax amesema serikali ya awamu ya sita imekuwa ikifanya jihada mbalimbali katika kuimarisha ushirikano na mataifa mbalimbali pamoja na masuala ya kidiplomasia.
“Leo hii tumekuwa na tukio la ufunguzi wa ofisi ya kuanzia ya ubalozi wa Ufaransa hapa Dodoma tunawashukuru sana kwa tukio hili lakini haya ni matokeo ya Rais Samia na jitihada zake za kutaka kuimarisha ushirikiano na mataifa mbalimbali na kurahisisha mawasiliano kati ya serikali yetu na mataifa mengine,”amesema.
Aidha, amesema serikali inaendelea na jitihada za kuboresha miundombinu mbalimbali mkoani hapa ili kuwezesha mabalozi ambao watakuwa tayari kuhamia kupata huduma zote bila kikwazo.
“Nilipoambiwa mnakuja leo na mnatumia uwanja huu wa ndege nikasema msifikilie kuwa huu ndiyo uwanja pekee tulio nao hapana tunajenga uwanja mkubwa sana wa ndege Msalato lakini pia tunaendelea kuboresha huduma nyingine kama vile ujenzi wa barabara,reli ,shule pamoja na huduma nyingine za kijamii ambazo mtaweza kuzitumia mkihamia hapa,”amesema.
Kadhalika, amewataka mabalozi kuunga mkoni jitihada za serikali ya awamu ya sita kuhamia makao makuu Dodoma kwa kuanzisha ofisi zao na serikali itakuwa mstari wa mbele kutoa ushirikiano kufanikisha jambo hilo.
“Niwahakikishie kuwa serikali kupitia wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki itaendelea kutoa ushirikiano mtakao uhitaji muda wote lakini pia kwa Balozi ambazo zitakuwa tayari kutaka kufungua ofisi zao jijini Dodoma tutazisaidia kufanya hivyo,”amesema.
Hata hivyo Dk. Tax amesema serikali inatambua jitihada mbalimbali za kimaendeleo ambazo zimekuwa zikifanywa na Ubalozi huo nchini katika sekta za nishati,maji pamoja na usafirishaji.
Naye, Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania Nabil Hajloui, amesema ufunguzi wa ofisi hiyo ni matunda ya Rais Samia Suluhu Hassan alipotembelea ofisi ya ubalozi huo alipofanya ziara mwaka jana nchini Ufaransa.
Amesema mataifa ya Tanzania na Ufaransa yamekuwa na ushirikiano wa kidiplomasia kwa muda mrefu hivyo kufunguliwa kwa ofisi hiyo ndogo jijini Dodoma kutaendeleza kuimarisha mahusinano yaliyopo kimataifa.
Leave a comment