MATOKEO ya utafiti uliofanywa na Taasisi ya TWAWEZA kati ya tarehe 18 Juni na 12 Julai 2022 kwa wahojiwa 3,000 waliopigiwa simu, yameonesha kuwa maoni ya wananchi kuhusu tozo za miamala ya fedha kwa njia ya simu yanatofautiana. Anaripoti Urumasalu Kisung’uda, TUDARCo … (endelea).
Kwa mujibu wa takwimu za matokeo hayo yaliyowasilishwa leo jijini Dar es salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa TWAWEZA, Aidan Eyakuze ni kwamba asilimia 67 ya wananchi wengi wanakubali kuwa tozo hiyo ni njia muhimu ya serikali kukusanya mapato na asilimia 63 wanaamini kwamba inasaidia kumfanya kila mtu achangie maendeleo ya taifa.
Aidha, asilimia 46 wamekubali kuwa tozo hiyo itapunguza utegemezi kwa wafadhili ambapo asilimia 43 wamekubali tozo za miamala ya fedha kwa njia ya simu ni kitu zuri.
Akiwasilisha mukhtasari wa matokeo hayo, amesema wananchi wanaonesha dalili kuwa wangeunga mkono zaidi tozo hizo iwapo wangekuwa na taarifa kamili kuhusu matumizi ya fedha zinazokusanywa kupitia tozo.
“Asilimia 63 wanasema wangekuwa tayari zaidi kulipa tozo iwapo wangeweza kufuatilia matumizi ya fedha hizo. Asilimia 39 wanasema wanajua pesa zinatumikaje na asilimia 44 wanasema wanaweza kutafuta kwa urahisi taarifa kutoka serikalini juu ya matumizi ya mapato ya tozo.
Aidha, amesema wananchi wanataja miradi mbalimbali ambayo wangependa yanufaike na tozo za miamala. Eneo la kwanza kabisa ni huduma za afya (57%) na elimu (50%), ikifuatiwa na ujenzi wa barabara (38%), huduma za maji (33%), umeme (20%), kilimo (18%) na mikopo (17%). Pia wamependekeza maeneo mengine mengi.
,”Maoni ya wananchi kuhusu tozo za miamala ya fedha kwa njia ya simu yanadhihirisha changamoto ya utawala. Serikali haina budi kupanua wigo wa kodi ili kuongeza mapato yatakayo gharamia huduma za jamii. Kupanua wigo wa walipakodi kunawashirikisha wananchi wengi zaidi kwenye mipango ya maedeleo na kuwafanya wadai uwajibikaji kwa serikali.
“Lakini huduma za fedha kwa njia ya simu zimesaidia sana kwenye biashara na mapato ya familia. Tozo zimepandisha gharama za huduma hizi muhimu, zimewafanya wananchi wapunguze kwa kiasi kikubwa matumizi ya huduma hizi na huenda zikaathiri ukusanyaji wa mapato,” aliendelea.
“Je, Serikali inapaswa kufanya nini kusawazisha mambo haya mawili yanayokinzana ili kujenga jamii yenye haki? Jibu mojawapo ni kuzisikiliza sauti za wananchi inapofanya maamuzi makubwa kama haya ya tozo. Usikivu wa serikali utasaidia kujenga imani ya wananchi, na kuiongeza ari yao ya kuchangia maendeleo kwa hali na mali.” alihitimisha.
Leave a comment