Friday , 26 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa TLS yatoa tamko kupinga mahabusu kufanyishwa kazi
Habari za Siasa

TLS yatoa tamko kupinga mahabusu kufanyishwa kazi

Spread the love

CHAMA cha Wanasheria Tanganyika (TLS) kimeiomba Serikali ya Tanzania, kusitisha mpango wake wa kufanyisha kazi mahabusu, kwa kuwa unakwenda kinyume na Katiba ya nchi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).

Tarehe 31 Mei 2020, Serikali ya Tanzania kupitia George Simbachawene, Waziri wa Mambo ya Ndani, alisema Serikali iko mbioni kuanzisha mfumo ambao utawawezesha mahabusu kufanya kazi, ikiwemo kazi za kilimo, ili wapate chakula.

Simbachawene alisema Serikali iko katika mjadala wa kuangalia namna gani mahabusu watafanya kazi tofauti na wafungwa, huku akisisitiza kwamba, hawatafanyishwa kazi za kutweza utu wao.

“Hatutaki kuwatumia kwa ajili ya kuwafanyisha kazi zinazotweza utu wao, wao wana adhabu wanazotumika lakini tunataka kuwatumia kuzalisha, tutawafanyisha kazi kama watu wengine wanavyofanya kazi hilo lazima lieleweke na sio tunataka kuwatumia mahabusu kama wafungwa,“ alisema Simbachawene

“Ingawa  kuna mjadala mkubwa, ila matumizi ya mahabusu na kuwaangalia huo mjadala bado upo tunaendelea kuchakata lakini tutakuja na majibu na mapendekezo kisha tutashirikiana, lakini tunataka kuwatumia kwa nia njema ya kuzalisha sababu imeandikwa katika vitabu vitakatifu asie fanya kazi na asile,” alisema

Dk. Rugemeleza Nshala, Rais wa TLS jana Ijumaa tarehe 5 Juni 2020 alitoa tamko akizungumzia kauli hiyo ya Waziri Simbachawene akisema, utekelezwaji wa mpango huo, utakuwa ni kinyume na misingi ya haki za binadamu.

“Nchi yetu inatakiwa kuwa katika mstari wa mbele katika kukuza, kuheshimiwa haki za watu na wanadamu na si kurudi katika zama za kikoloni ambapo mtuhumiwa hakuthaminiwa kwa kuchukuliwa kama mkosaji, hadi hapo atakapothibitishwa hana hatia,” alisema Dk. Nshala

“Kumfanyisha kazi mahabusu ni kumtweza mtu na kumpa adhabu wakati bado hajatiwa hatiani na kunaweza kuchagiza kuwekwa ndani watu wengi kwa makosa ya kuwabambikia, ili kuwakomoa na kuwatweza.”

Dk. Nshala alisema, “hilo ni kosa kubwa ambalo historia haitotusamehe wote kwa kuliruhusu kuwa sehemu ya sheria zetu.”

Aliitaka Serikali ya Tanzania, kuboresha mfumo wa utoaji haki, ili kupunguza gharama za kuwahudumia mahabusu, badala ya kuwafanyisha kazi ili wajihudumie wenyewe.

“TLS tunaitaka Serikali kusitisha mara moja mpango wake badala yake ijikite katika kuboresha mfumo wa utoaji haki, kwa haraka ili kupunguza gharama za kuwahudumia mahabusu,” alisema Dk. Nshala.

TLS ilisema,  njia nzuri ya kuwa na watuhumiwa wa makosa ya jinai ambao wanajitafutia chakula chao cha kila siku ni kuhakikisha watuhumiwa wanapata dhamana.

“Dhamana iwe haki ya kila mtuhumiwa. Sheria zote ambazo zinazuia kutolewa kwa dhamana kwa watuhumiwa zifanyiwe marekebisho na ikiwa ni pamoja na makosa ya uhujumu uchumi, utakatishaji fedha na makosa yote yaliyoainishwa na kifungu cha 148(5)(a)(i) –(vi)-(e) cha Sheria ya Mwenendo wa Jinai Namba 20 kama ilivyorejewa Mwaka 2002,” alisema Dk. Nshala

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Prof. Muhongo akomalia matumizi nishati jadidifu kuondoa uhaba wa umeme

Spread the love  MBUNGE wa Musoma Vijijini (CCM), Profesa Sospeter Muhongo, ameendelea...

Habari za Siasa

Kilosa yawa mfano wa kuigwa miradi ya Mwenge nchini

Spread the love  KIONGOZI wa Mbio za Mwenge Kitaifa Godfrey Mzava amezitaka...

Habari za SiasaTangulizi

Biteko ataja vipaumbele 7 bajeti nishati 2024/25

Spread the love  NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto...

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

Mwekezaji amwaga bil. 39 kujenga viwanda 3 vya uchenjuaji

Spread the loveKampuni ya Mineral Access System Limited (MAST) inayoiwakilishwa kampuni ya...

error: Content is protected !!