SIKU moja tu kufuatia kauli ya Msemaji wa klabu ya Simba, Haji Manara ya kutotaka mashabiki wa timu pinzani kuingia Uwanjani kwenye mchezo dhidi ya Plateau, Shirikisho la Mpira wa Miguu TANZANIA (TFF) imekemea kwa nguvu kauli hiyo kutokana na suala la ubaguzi kutokubalika kwenye mchezo wa mpira wa miguu. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Katika mkutano wake na waandishi wa habari, Manara alisema kuwa katika mchezo huo wa siku ya Jumamosi tarehe 5 Desemba, 2020, hawatoruhusu jezi isiyokuwa rangi nyekundu na nyeupe au mashabiki wasiokuwa wao kuingia uwanjani kwa kuwa mchezo huo ni wao.
Kauli hiyo ya msemaji huyo imekuja mara baada ya mashabiki wa Yanga ambao ni wapinzani wao kuonekana kutaka kwenda kuwashabikia wageni hao na hata baadhi yao kuonekana kununua na kuvaa jezi ya timu hiyo ambayo ni mabingwa wa Ligi Kuu nchini Nigeria.
Taarifa kutoka ndani ya TFF imeeleza kuwa kwa mujibu wa katiba ya Shirikisho la Mpira Dunia (Fifa) na TFF vitendo vyovyote vya ubaguzi havikubariki kwenye mpira wa miguu.
Aidha taarifa hiyo imeendelea kueleza kuwa shabiki yoyote anaruhusiwa kuingia kwenye mechi ya mpira wa miguu ikiwa tu hatovunja sheria na taratibu.
Simba itashuka uwanjani siku hiyo kucheza mchezo wa klabu bingwa barani Afrika kwenye hatua ya awali dhidi ya Plateau kwenye mchezo wa mzunguko wa pili mara baada ya kuibuka na ushindi wa bao 1-0, kwenye mchezo wa kwanza uliochezwa mjini Jos, Nigeria.
Leave a comment