JUKWAA la Wahariri Tanzania (TEF), limesema mwaka 2023 utakuwa mwaka wa mageuzi katika sekta ya habari kwa kuwa marekebisho ya Sheria ya Huduma za Habari ya 2016 yatakamilika, pamoja na mchakato wa marekebisho ya Sera ya Habari na Utangazaji ya 2003, utaanza. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Balile ametoa kauli hiyo leo Alhamisi tarehe 5 Januari 2023, akizungumza na mtandao wa MwanaHalisi Online.
“Ni matarajio yetu kwamba mwaka huu wa 2023 utaleta mageuzi katika tasnia ya habari, sisi huku kwenye mikutano ya wadau tumeshamaliza kazi yetu ambapo kikao cha mwisho tulifanya tarehe 21 Novemba 2022, baadae tukaongeza na Kongamano la Maendeleo ya Sekta ya Habari 2022 lililofanyika tarehe 18 Desemba 2022. Hivyo kilichobaki ni Muswada wa Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari ya mwaka 2016 kuwasilishwa bungeni baadae mwezi huu,” amesema Balile.
Mwenyekiti huyo wa TEF amesema, wadau wanatarajia kuona maoni na mapendekezo iliyowasilisha serikalini yatazingatiwa katika marekebisho hayo.
Balile amesema matarajio ya wadau wa habari ni kuona muswada huo wa mabadiliko ya sheria unasomwa bungeni tarehe 31 Januari 31 2023, kufuatia ahadi iliyotolewa na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, Nape Nnauye, kwamba utawasilishwa katika bunge linaloanza mwezi huu.
“Kwanza kabisa utapitia kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, kisha utajadiliwa na Kamati ya Makatibu Wakuu na baada ya hapo utajadiliwa na Kamati ya Baraza la Mawaziri. Ukitoka hapo utajadiliwa na Baraza la Mawaziri, tunarajia itakuwa kati ya Januari 13 na 14, matazamio yetu ni kwamba utasomwa bungeni kwa mara ya kwanza Januari 31, mwaka huu kisha tutakutana na wadau kuzungumza na wabunge baadae utasomwa kwa mara ya pili na utajadiliwa,” amesema Balile.
Naye Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Dar es Salaam (DCPC), Samson Kamalamo, hivi karibuni alisema mabadiliko ya Sheria ya Huduma za Habari itakuwa mwanzo wa kutafuta ufumbuzi wa matatizo yaliyopo katika sekta ya habari.
“Hii haitakuwa mwarobaini, isipokuwa itakuwa mwanzo wa kutafuta ufumbuzi wa matatizo yaliyopo katika sekta ya habari na kuiboresha. Lakini pia, tujifunze kwa wenzetu wamefanikiwa vipi, tusijifungie ndani,” alisema Kamalamo.
Tarehe 18 Disemba 1 2022 akizungumza katika Kongamano la Maendeleo ya Sekta ya Habari 2022, Nape alisema Serikali ina mpango wa kurekebisha sekta ya habari kupitia mfumo wa kisheria, ikiwa ni pamoja na kuunganisha Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari ya mwaka 2016 na Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta ya mwaka 2010.
Waziri Nape alisema hatua hiyo inatarajiwa kuleta uratibu madhubuti wa sekta hiyo na umoja kati ya wahusika katika magazeti, mitandao ya elektroniki na kijamii kwa kuwa zote ziko chini yake.
Leave a comment