SERIKALI imetaja sababu za Tanzania kushuka kwa nafasi tano, kutoka nafasi ya pili hadi ya nane katika orodha ya nchi zenye vivutio vya asili duniani. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Akijibu swali la Mbunge wa Vunjo, James Mbatia leo tarehe 21 Mei 2019 bungeni jijini Dar es Salaam, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamiss Kigwangalla amesema Tanzania imeshuka kutokana na uharibifu wa mazingira katika maeneo ya vivutio vya utalii.
Katika swali lake, Mbatia ameuliza Tanzania inashika nafasi ya ngapi kwenye orodha ya nchi yenye vivutio vya asili na miundombinu mizuri ya kuvutia watalii duniani?
Dk. Kigwangalla amesema, uharibifu wa mazingira na uvamizi wa mifugo pamoja na shughuli za kibinadamu katika maeneo ya vivutio ndiyo chanzo cha Tanzania kushuka, na kwamba kwa sasa serikali inakabiliana na changamoto hiyo.
“Utafiti uliofanyika mwaka 2012 hadi 2014 ulitoa taarifa kuwa, Tanzania inashika nafasi ya pili kwa vivutio vya asili duniani. Kutokea kipindi hicho hadi sasa haujafanyika utafiti mwingine, lakini matokeo ya katikati yalitoka ilionekana imeshuka kutoka nafasi ya 2 hadi 8,” amesema Dk. Kigwangalla na kuongeza;
“Sababu uharibifu wa mazingira, uvamizi wa mifugo na makazi katika maeneo ya vivutio vya utalii vya asili. Kazi kubwa kuondoa wavamizi na kupandisha hadhi maeneo, inaweza ikapandisha zaidi kwenye ubora wa vivutio vya utalii duniani.”
Leave a comment