SERIKALI imebaini kuwa baadhi ya wafanyabiashara wamepandisha gharama za bidhaa mbalimbali mara tatu ya bei halisi.
Pia imebaini kuwa kuna baadhi ya wafanyabiashara wanaficha bidhaa ili watengeneze uhaba wa bidhaa. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Hayo yameelezwa leo tarehe 13 Februari, 2022 na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa wakati akijibu swali la mwananchi aliyempigia simu kutaka kufahamu hatua zilizochukuliwa na serikali kuthibiti kupanda kwa bei za bidhaa hususa vifaa vya ujenzi.
Msigwa ambaye amefanya mkutano na waandishi wa habari Visiwani Zanzibar amesema serikali ipo macho na inafuatilia wafanyabiashata hao hivyo watakapobainika watafikisha kwenmye vyombo vya sheria.
Amesema hayo yamebainika kutokana na uchunguzi unaofanywa na kamati iliyoundwa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, kuchunguza sababu za kupanda kwa bei za bidhaa.
“Serikali imefanyika kazi na Waziri Mkuu, juzi (tarehe 11 Februari, 2022) ametoa maelekezo ya kuunda timu ya kufanya uchunguzi kwa wafanyabiashara wote ambao wamekuwa na tabia ya kupandisha bei kupita kiasi hawana sababu za msingi.
“Kwa sababu Serikali imefanya utafiti imepita katika maeneo ya uzalishaji, maeneo ya viwandani na hata maeneo ya wasambazaji wakubwa wa bidhaa.
“Tumebaini kwamba wako baadhi ya wafanyabiashara ambao wanapandisha gharama mara tatu ya bei halisi, serikali imeanza kuwachunguza na nitoe rai kwa wafanyabiashara wote wanaofanya mchezo huo kuacha mara moja,” amesema.
Amesema kwa kuwa sheria zipo, kamati hiyo ikimkamata mtuhumiwa atachukuliwa hatua za kisheria.
“Tayari serikali imeshaunda kamati ambayo inafanya uchunguzi huu na wote watakaobainika watafikishwa mbele ya vyombo vya sheria.
“Pamoja na gharama kupanda za bidhaa mbalimbali lakini ziwe gharama halisi, sio mtu kwa sababu umeona gharama zimepanda unaamua kupandisha mara nyingi upate faida kubwa.
“Lakini pia kuna watu wanaficha bidhaa ili watengeneze uhaba serikali inafuatilia ipo macho, tukiwabaini nao tutawafikisha kwenmye vyombo vya sheria,” amesema.
Aidha, amesema mojawapo ya sababu ya bei za bidhaa kupanda duniani ni pamoja na janga la maambukizi ya virusi vya Corona.
“Bidhaa nyingi zimepanda bei hasa kwa sababu gharama za uzalishaji zimepanda, kwa hiyo vifaa vingi hasa tunavyoingiza kutoka nje ya nchi vimpenda bei na hiyo imetokea hata kwenye masoko yetu na maduka tunakonunua hasa vifaa vya ujenzi.
“Lakini sasa bei ya vifaa vya ujenzi imeanza kupungua, leo nimeuliza bei ya tani moja ya nondo… imeshuka hadi Sh milioni 2.4 wakati ilikuwa imefika milioni 2.8 kwa tani moja,” amesema.
Leave a comment