RAIS wa Senegal, Macky Sall ametangaza leo Jumatatu tarehe 7 Februari, 2022 kuwa siku ya mapumziko kusherehekea ushindi wa timu ya taifa wa Kombe la Mataifa ya Afrika (Afcon). Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Rais Sall ambaye alikuwa nje ya nchi amefutilia mbali awamu ya mwisho ya safari yake katika Visiwa vya Comoro na kurejea nchini mwake kuwapokea nyota hao wa soka kurejea nchini leo.
Kwa mujibu wa Televisheni ya Taifa – RTS, Rais Sall pia kesho Jumanne ataiandalia dhifa maalumu Ikulu.
Senegal imeshinda fainali ya kwanza ya Afcon baada ya kushindwa mara mbili katika fainali za mwaka 2002 na 2019.
Waliishinda Misri 4-2 kwa mikwaju ya penalti na kupata ushindi wao baada ya fainali kumalizika bila bao kufuatia muda wa nyongeza.
Wakati huo huo, raia wameendelea kusherehekea usiku kucha kuamkia leo Jumatatu katika miji mbalimbali nchini Senegal kufuatia ushindia wa Kombe la Mataifa ya Afrika.
Kocha wa Senegal Aliou Cissé kipindi akiwa mchezaji alikosa penalti muhimu fainali za mwaka 2002 na kushindwa kubeba kombe hilo la Afcon.
Akiwa kama kocha, timu hiyo ilishindwa katika fainali ya mwaka 2019.
Senegal na Misri zitakutana tena katika mechi nyingine mwezi ujao kwenye mchujo wa kuwania kufuzu kwa Kombe la Dunia 2022 nchini Qatar.
Leave a comment