ZIKIWA zimebaki siku 12 kuelekea siku ya maadhimisho wa wiki ya sheria, Mahakama nchini imesema itaendelea kutoa haki kwa wakati na kwa gharama nafuu. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam …(endelea).
Hayo yamesemwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma alipokuwa akitoa taarifa kwa waandishi wa habari leo tarehe 10 Januari, 2023 kuhusu maandalizi ya siku hiyo ya sheria nchini. Amesema kuwa mahakama itaendeleza mpango wake wa kutoa haki kwa wakati.
Prof. Juma amesema maadhimisho ya wiki hiyo yataanza tarehe 22 Januari hadi tarehe 29 Januari ambapo kilele cha maadhimisho hayo kitafanyika tarehe 1 Februali 2023 katika viwanja vya Chinangali, Jijini Dodoma ambapo Rais Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.
Wiki ya sheria itafunguliwa kwa matembezi yatakayofanyika siku ya Jumapili tarehe 22 Januari, 2023 saa 12 asubuhi ambapo mgeni rasmi kwenye matembezi hayo anatarajiwa kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Phillip Mpango.
Amesema matembezi hayo yataanzia Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma na kuishia kwenye Viwanja vya Nyerere Square Jijini Dodoma.
Profesa Juma amesema kauli mbiu ya siku hiyo ni “umuhimu wa utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi katika kukuza uchumi endelevu: Wajibu wa mahakama na wadau.’’
”Kauli mbiu hii imebeba ujumbe mahususi kuhusu wajibu wa Mahakama na wadau wake katika kutumia njia ya usuluhushi kutatua migogoro kwa lengo la kukuza uchumi endelevu” amesema Prof. Juma.
Amesema maadhimisho hayo yatabeba malengo sita ya mahakama ambayo ni:- Upatikanaji wa haki kwa wakati na kwa gharama nafuu, kupunguza mirundikano ya mashauri Mahakamani, kuimarisha amani na ustawi wa Jamii, kutumia muda mfupi kushughulikia migogoro na kubaki na muda mwingi zaidi katika shughuli za uzalishaji mali na utoaji huduma.
Nyingine ni kulinda mahusiano ya wadaiwa kijamii na kiuchumi, kuhifadhi na kuendeleza mahusiano ya kibiashara na ya kijamii.
Aidha, Prof. Juma ametoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi ili kupata elimu juu ya masuala ya sheria na haki.
”Nitumie fursa hii kuwahimiza wananchi wa mkoa wa Dodoma ambako maonesho ya wiki ya sheria kitaifa yatafanyika wafike kwenye viwanja vya Nyerere Square ili wapate elimu mahsusi kuhusu utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi. Lakini pia wananchi watakaofika kwenye viwanja hivyo watapata nafasi ya kutoa malalamiko, maoni na mapendekezo ya uboreshaji wa huduma za Mahakama,” amesema.
Leave a comment