RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amesema hivi karibuni atafanya mabadiliko ya viongozi wa wilaya nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza…(endelea).
Viongozi hao ni Wakuu wa Wilaya (DC), Wakurugenzi (DED) na Makatibu Tawala (DAS).
Rais Samia alitoa taarifa hiyo jana Jumanne, tarehe 15 Juni 2021, akizungumza na vijana wa Tanzania, jijini Mwanza.
Akizungumza katika mkutano huo, Rais Samia alisema mkeka wa mabadiliko ya viongozi hao, utatoka hivi karibuni, baada ya mkeka wa Makatibu Tawala wa Mikoa (RAS), kutoka.
Kiongozi huyo wa Tanzania, alifanya mabadiliko ya Ma-RAS, tarehe 30 Mei 2021, kwa kuteua wapya 11 na kuwahamisha tisa, huku sita wakibaki katika mikoa yao.
“Karibuni nimeteua Ma-RAS, kuna mkeka wa Ma-DC utakaotoka karibuni. Mbali ya mkeka wa Ma-DC, bado nina mkeka wa wakurugenzi na Ma-DAS haujatoka,” alisema Rais Samia.
Rais Samia alitoa wito kwa vijana nchini, kuchangamkia fursa hizo, huku akiwataka wasiwaangushe watu wanaowateua.
“Nataka kuwaambia wote ni vijana, kwa hiyo hizo ndizo fursa mlizonazo vijana, ingawa baadhi yenu tunapowapa fursa hizi mnakwenda kufanya mnavyofanya na kutuangusha. Ningeomba mnapopata fursa hii mkazitumikie kwa umakini,” amesema Rais Samia.
Leave a comment