RAIS wa Jamhuri ya Muungano, John Pombe Magufuli, amekacha kuhudhuria sherehe za kuapishwa kwa Rais wa Kenya, Uhuru Kenyetta, zinazofanyika mjini Nairobi, leo Jumanne. Anaripoti Mwanadishi Wetu.
Taarifa kutoka Ikulu jijini Dar es Salaam na Nairobi nchni Kenya zinasema, kiongozi huyo wa Tanzania ameamua kumtuma makamu wake wa rais, Samia Suluhu. Awali Rais Magufuli alithibitisha kuhudhuria sherehe hizo.
Katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Twiter, Rais Magufuli amesema, hakwenda kwenye tukio hilo kutokana na alichokiita, “sababu zake binafsi.”
Katika siku za hivi karibuni, uhusiano kati ya Kenya na Tanzania umeonekana kudorora kufuatia kupigwa mnada kwa ng’ombe zaidi ya elfu moja kutoka Kenya waliokuwa wameingizwa nchini; kuchomwa moto kwa vifaranga wa kuku waliodaiwa kutoka Kenya na kuwapo kwa “uswahiba” wa karibu kati ya Rais Magufuli na kiongozi wa upinzani nchini humo, Raila Odinga.
Tayari kiongozi wa upinzani nchini, Edward Lowassa ambaye ni rafiki mkubwa wa rais Kenyatta amewasili katika uwanja wa Kasarani kwa ajili ya sherehe hiyo.
Rais Magufuli ni mwandani wa karibu wa Odinga aliyesusia uchaguzi wa marudio wa 26 Oktoba mwaka huu, ambao Rais Kenyatta aliibuka mshindi kwa kujipatia asilimia 98 ya kura zilizopigwa.
Leave a comment