SERIKALI nchini Tanzania imesema imefanikiwa kuwapatia vijana 45,047 mafunzo ya ukakamavu, stadi za kazi, kuwajengea uzalendo na umoja wa kitaifa katika operesheni Samia Suluhu Hassan. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Hayo yameelezwa leo Alhamisi tarehe 19 Mei, 2022 bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk. Stergomena Tax akiwasilisha bajeti yam waka 2022/23.
Amesema katika kipindi husika mafunzo kwa Vijana wa Mujibu wa Sheria na Kujitolea yamefanyika kwenye Kambi mbalimbali za Jeshi la Kujenga Taifa.
Amefafanua jumla ya vijana 25,503 wa Mujibu wa Sheria wamepatiwa mafunzo na kati yao 19,544 ni wa kiume na 5,959 ni wa kike.
Aidha, amesema vijana 11,739 wa Kujitolea wamepatiwa mafunzo na kati yao 8,165 ni wa kiume na 3,574 ni wa kike.
“Napenda kutumia fursa hii kuliarifu Bunge lako Tukufu pamoja na umma wa watanzania kwamba, dhumuni la mafunzo yanayotolewa kwa vijana ni kuwapatia stadi za kazi na stadi za maisha ili baada ya kumaliza muda wa mafunzo na kutumikia Jeshi la Kujenga Taifa, waweze kurejea majumbani kwao wakiwa raia wema wenye uwezo wa kujitegemea na kulilinda Taifa.
“Nitoe rai kwa vijana wote wanaopata fursa za kupata mafunzo hayo kuzitumia stadi za kazi walizozipata kujiajiri na kujitegemea.” Amesema Dk. Tax.
Leave a comment