MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, imewasomea mashtaka watu wawili kwa kosa la kuchapisha maudhui mtandaoni bila leseni kutoka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea)
Washitakiwa hao ni Mwanafunzi wa Chuo cha Biashara (CBE), Isaya Masawe (21) na Ofisa Habari Msaidizi wa CHADEMA, Dominic Mgaya ambao wamesomewa mashitaka kwa mahakimu wawili tofauti leo Ijumaa tarehe 18 Septemba 2020.
Mshitakiwa Mgaya amesomewa mashitaka mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Richard Kabate na Wakili wa serikali Adolph Ulaya ambapo alidai mshitakiwa alitenda kosa hilo katika tarehe tofauti 14 Oktoba mwaka 2017 hadi tarehe 1 Septemba mwaka 2020 jijini Dar es Salaam.
Ilidaiwa, mshitakiwa alirusha maudhui hayo kupitia chaneli ya Youtube iitwayo Chadema Media TV bila leseni kutoka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA ).
Mshitakiwa huyo aliachiwa kwa dhamana baada ya kutimiza sharti la kuwa na wadhamini waliosaini bondi ya Sh. 500,000 kila mmoja. Kesi iliahirishwa hadi tarehe 20 Oktoba 2020.
Wakili wa Serikali, Adolph Ulaya alidai kati ya tarehe 4 February 2019 na 16, Septemba 2020 katika maeneo tofauti jijini Dar es salaam mshtakiwa huyo alichapisha maudhui mtandaoni kupitia channel ya YouTube Kwa jina la Isaya Thomas Masawe bila ya kupata leseni kutoka TCRA.
Mshtakiwa huyo alikana shitaka linalomkabili huku upelelezi bado haujakamilika.
Baada ya maelezo hayo, Hakimu Yusto Ruboroga alisema dhamana ipo wazi kwa mshtakiwa huyo hivyo anatakiwa apate wadhamini wawili ambao wenye vigezo vyote na watasaini dhamana ya Sh. 3 million.
Mshtakiwa huyo alikidhi vigezo na akaachiwa kwa dhamana kesi hiyo itasikilizwa tarehe 15 Oktoba 2020.
Leave a comment