KATIKA kuuunga mkono juhudi za Serikali kuwainua vijana kupitia mradi wa kuwawezesha kulima, kuvua na kufuga kibiashara (BBT), Benki ya NMB imetenga jumla ya Sh bilioni 20 pamoja na kuwaelimisha vijana hao namna ya kupata mikopo hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mbeya…(endelea).
Pia NMB imetenga Sh bilioni 20 kwa ajili ya ujenzi wa maghala ya kuhifadhi mazao ya wakulima ambapo kwa kipindi cha miaka miwili iliyopita jumla ya bilioni saba tayari zimekwishatolewa.
Hayo yameelezwa leo tarehe 3 Agosti 2023 na Meneja wa Kanda ya Nyanda za Juu, Straton Chilongola alipokuwa akimweleza Waziri Mkuu Kassim Majawali namna benki hiyo inavyotoa kipaumbele kwenye sekta ya kilimo ambayo ndio uti wa mgongo wa Taifa.
Waziri Mkuu ametembelea banda la NMB katika Maonesho ya Nanenane yanayofanyika kwenye viwanja vya John Mwakangale mkoani Mbeya.
Chilongola amesema pamoja na mambo mengine pia benki hiyo inatoa huduma ya mikopo (NMB mshiko fasta), ambapo wakulima wanaweza kukopa hadi Sh 500,000 kupitia simu za kiganja bila dhamana wala kufika kwenye matawi ya benki hiyo.
Amesema benki hiyo pia ni ya kwanza nchini kushusha riba kwa wakulima na wafugaji hadi kufikia asilimia tisa.
Waziri Mkuu ambaye alikuwa ameongozana na Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdalah Ulega aliipongeza NMB kwa huduma hizo ambazo zinazidi kuinua pato la Mtanzania.
Aidha, Ulega alikiri kuwepo mikopo hiyo ya BBT ambapo aliongeza kuwa maofisa kutoka NMB wametoa elimu namna vijana wanavyoweza kukopa.
Amesema mafunzo hayo yametolewa katika vituo vya Tanga, Mwanza na Kagera ambapo maofisa hao waliwawezesha vijana namna ya kuandaa maandiko ya mikopo.
Leave a comment