MASHIRIKA Yasiyo ya Kiserikali (NGO’s) na Asasi za Kiraia (AZAKI) 1,500, zinatarajia kushiriki maonesho ya wiki ya asasi hizo, yanayotarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 23 hadi 29 Oktoba 2021, jijini Dodoma. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa foundation for civil society (FCS), Francis Kiwanga, akizungumza na wanahabari, leo Alhamisi, tarehe 12 Agosti 2021, jijini Dodoma.
Kiwanga amesema, lengo la maonesho hayo ni kuionesha Serikali na jamii, kazi zinazofanywa na AZAKI, katika kuleta maendeleo ya wananchi.
Amesema mijadala na midahalo mbalimbali, itaendeshwa katika wiki hiyo ya AZAKI.
“Wiki ya Azaki inatarajiwa kuanza kufanyika Oktoba 23 hadi 29 mwaka huu, katika Uwanja wa Jamhuri jijini hapa. Tunategemea Asasi za Kiraia zitatumia fursa hii kutengeneza malengo yao mahsusi kwa manufaa ya jamii ya watanzania,”amesema Kiwanga.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Hakirasilimali, Rachel Chagonja, amesema tayari maandalizi ya wiki ya AZAKI yamekamilika.
Chagonja amewaomba wananchi kushiriki moja kwa moja katika maonyesho ya wiki hiyo, ili kujifunza masuala mbalimbali, yahusuyo masuala ya kisheria, haki za binadamu na afya.
“Tuna jumla ya Asasi 1,500 ambazo tayari zimethibitisha kushiriki wiki ya Asasi za kiraia, kupitia asasi hizo masuala mengi yanafanyika ambayo pengine jamii haiyajui. Nitoe rai kwa jamii kuchangamkia fursa hiyo kujifunza,”amesema Chagonja.
Leave a comment