BAADA ya kuteuliwa na kuapishwa kuwa Skauti Mkuu wa Chama cha Maskauti Tanzania, Mwantumu Mahiza ameahidi kuieneza skauti katika vyuo vya kati na vyuo vikuu. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Mahiza ameyaahidi hayo leo tarehe 3 Oktoba 2018 ikulu jijini Dar es Salaam, ambapo alimhakikishia Rais John Magufuli kwamba atautumia vyema wadhifa huo katika kujenga maadili ya vijana wa kitanzania.
Mahiza ameeleza kuwa, kwa miaka mingi skauti ilienea katika shule za msingi na sekondari na kwamba ni wakati husika kwa taasisi hiyo ya kujenga maadili ya vijana wa Tanzania kuenea katika vyuo vyote hapa nchini.
“Nakushukuru kwa kuniteua kulea vijana wa Tanzania kupitia skauti, wajibu wangu ni mambo mawili, kuhakikisha skauti inaenea katika vyuo vya kati na vyuo vikuu kwa sababu miaka mingi ilienea shule za msingi na sekondari,” amesema Mahiza.
Katika hatua nyingine, Mahiza aliahidi kufanikisha ujenzi wa kambi ya kimataifa ya Skauti jijini Dodoma.
Leave a comment