MWANDISHI wa habari na mpiga picha wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) mkoani Manyara Joachim Kapembe amefariki dunia alipokuwa akishuka kutoka katika kilele cha Mlima Kilimanjaro. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo tarehe 14 Disemba, 2022 na Shirika hilo, Kapembe amefariki jana tarehe 13 Disemba, 2022.
Imesema Kapembe pamoja na watendaji wengine wa wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari walipanda kwenye mlima Kilimanjaro tarehe 9 Disemba, 2022 kwa ajili uzinduzi wa intaneti ya mwendokasi ya Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL).
Mwandishi huyo, alizaliwa tarehe 26 Februari mwaka 1977 wilayani Muheza mkoani Tanga.
Aliajiriwa na TBC Oktoba Mosi mwaka 2011 kwa cheo cha mpiga picha daraja la II.
Hadi anafariki dunia tarehe 13 mwezi huu alikuwa na cheo cha mpiga picha mkuu daraja la I.
Joachim Kapembe ameacha mke na watoto wawili.
Leave a comment