MTUMISHI wa Afya anayefahamika kwa jina la Sarah, amenaswa akiuza dawa za serikali katika duka lake la dawa za binadamu (Pharmacy) lililoko katika Kata ya Ibelamilundi wilayani Uyui mkoa wa Tabora. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Muuguzi huyo alinaswa baada ya Mkuu wa Wilaya ya Uyui, Gifti Msuya pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya hiyo kufanya ziara ya kushtukiza katika duka lake usiku wa jana tarehe 15 Aprili 2019.
Akizungumzia kuhusu tukio hilo, Msuya amesema walifanya ziara hiyo ya kushtukiza baada ya kupata taarifa kutoka kwa msamaria mwema ambaye hakumtaja jina.
“Tulipata taarifa hizi kutoka kwa msamaria mwema ambaye alinipigia simu baada ya kushtukia hujuma hiyo,” amesema Msuya.
Msuya ameeleza kuwa, Sarah ambaye ni muuguzi, katika nyakati tofauti amekuwa na tabia ya kuhamisha dawa za serikali katika duka lake la dawa, pindi anapokabidhiwa kwa ajili ya zahanati ya serikali.
Amesema Jeshi la Polisi linaendelea na taratibu za kisheria kwa ajili ya kumfikisha muuguzi huyo katika vyombo vya sheria.
“Mtumishi huyu hatuwezi kumuacha kwa hili alilolifanya. Na pia anaweza kupoteza kazi yake,” amesema Msuya.
Leave a comment