SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO) limetangaza kuzimwa kwa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa Kilovoti 220 Kidatu -Kihansi kwa tarehe 26 hadi 28 Agosti 2023
kuanzia saa moja kamili asubuhi hadi saa 12 kamili jioni (01:00 -12:00). Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea)
Taarifa iliyotolewa jana Ijumaa na shirika hilo imetaja sababu ya kuzimwa kwa njia hiyo kuwa ni kuruhusu Mkandarasi anayejenga kituo kipya cha kupoza umeme Ifakara kuunganisha kituo hicho kwenye gridi ya Taifa.
Imesema kazi hiyo itahusisha kuunga njia ya msongo wa Kilovoti 220 Kihansi -Kidatu kwenye kituo kipya.
“Kuunganishwa kwa kituo hiki kipya ni muhimu kwani kutasaidia kuongeza ubora na upatikanaji wa umeme katika wilaya za Kilombero, Ulanga na maeneo ya jirani sambamba na kuvutia wawekezaji,” imesema.
Taarifa hiyo imesema, kutokana na kazi hii baadhi ya maeneo kwenye mikoa yataathirika kwa awamu katika nyakati tofauti, ratiba kamili itatolewa kwenye Mikoa ya Iringa, Njombe, Ruvuma, Mbeya, Songwe, Dodoma, Singida, Manyara, Arusha, Kilimanjaro, Shinyanga, Simiyu, Tabora, Mwanza, Geita na Mara.
“Tutaendelea kuwafahamisha maendeleo ya kazi hiyo hadi kukamilika kwake,” imesema.
Leave a comment