WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Dk. Damas Ndumbaro, amesema Askari wa Hifadhi za Wanyamapori 61 wamefukuzwa kazi, huku 40 wakisimamishwa kupisha uchunguzi wa tuhuma zinazowakabili, ikiwemo kukiuka maadili yao ya kazi na kuanzisha migogoro baina ya wananchi na hifadhi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Dk. Ndumbaro ameyasema hayo leo Jumamosi, tarehe 5 Juni 2021, bungeni jijini Dodoma ,akijibu malalamiko ya wabunge kuhusu migogoro hiyo, katika mjadala wa Bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mwaka wa fedha wa 2021/2022.
“Wizara tumeanza kuchukua hatua, askari 61 tumewafukuza kazi na askari 40 wamesimamishwa kazi kupisha uchunguzi. Moja kati ya kazi ya kwanza mimi kufanya, ni kwenda Ifakara mkoani Morogoro, kufukuza kazi askari watatu,” amesema Dk. Ndumbaro.
Dk. Ndumbaro ametoa wito kwa wananchi wanaofanyiwa vitendo vya ukiukwaji haki za binadamu na askari hao, watoe taarifa kwa ajili ya Serikali kuchukua hatua.
“Mkakati wetu ni rahisi kutokomeza vitendo hivyo, tukipata malalamiko yenye ushahidi usio na shaka tunaitisha paredi tunamfukuza. Hatupendi askari aliyepata mafunzo anakiuka miiko ya kazi yake, tunachohitaji ushirikiano kutoka kwa wananchi na wabunge,” amesema Dk. Ndumbaro.
Dk. Ndumbaro amesema, kuanzia Julai Mosi 2021, Askari wa Hifadhi za Wanayamapori watakaobainika kukiuka maadili yao ya kazi na kusababisha migogoro, watapelekwa katika Mahakama za Kijeshi, kwa ajili ya kuchukuliwa hatua.
“Ninasaini kanuni hizo Jumatatu tarehe 7 Juni 2021, ili kuanzia tarehe 1 Julai askari atakayekiuka miiko ya kazi haendi kwenye mahakama za kawaida, anaenda mahakama za kijeshi na anafukuzwa kazi mara moja. Hii naamini italeta ufumbuzi kwenye hoja hii,” amesema Dk. Ndumbaro.
Leave a comment