TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoa wa Kinondoni imemfikisha mahakamani aliyekuwa Mhasibu Mwandamizi wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA), Isaya Paul Phillip pamoja na watumishi 11 wa benki ya CRDB wanaotuhumiwa kuisababishia hasara serikali. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Watuhumiwa hao wanaodaiwa kufanya makosa 404 ikiwemo la kuisababishia serikali hasara ya zaidi ya Sh. 569 milioni katika kipindi cha mwaka 2010 na 2013, wamefikishwa mahakamani na TAKUKURU leo tarehe 8 Oktoba 2018.
Akizungumza na wanahabari leo jijini Dar es Salaam, Naibu Mkuu Takukuru mkoa wa Kinondoni, Euginius Hazinamwisho amedai kuwa, watuhumiwa hao wamefikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili chini ya kifungu cha sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa namba 11 ya mwaka 2017 pamoja na sheria ya kanuni za adhabu ya sheria ya uhujumu uchumi sura ya 200 iliyorekebishwa mwaka 2002. Baada ya uchunguzi dhidi yao kukamilika.
Hazinamwisho amewataja watuhumiwa wengine, ikiwemo Adelphina Barongo, Daniel Kahamba, Edina Luiza, Ally Hamad, Msafiri Abdallah, Anthony Festo, Aisha Mussa na Hadija Selemani.
“Watuhumiwa hao leo wamefikishwa mahakamani mbele ya Hakimu Moshi, kwa makosa 404 ikiwa ni pamoja na kuisababishia hasara serikali zaidi ya milioni 539 fedha za Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA).
“Tumeona ni suala la msingi kuhabarisha wananchi wajue ofisi yao mambo inayofanya katika kutekeleza majukumu yake, wananchi wajue madhara ya matendo ya rushwa na matokeo yake waweze kujirekebisha kitabia,” amesema.
Katika hatua nyingine, Hazinamwisho amewataka watumishi wa umma na wa sekta binafsi hasa wa taasisi za fedha kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia kanuni na taratibu pamoja na kujiepusha na vitendo vya rushwa.
Leave a comment