Mgombea wa upinzani nchini Senegal, Bassirou Diomaye Faye ameonekana kuongoza katika matokeo ya awali ya uchaguzi wa rais ambao ulifanyika jana Jumapili baada ya miaka kadhaa ya ghasia na mzozo wa kisiasa. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Mshindi wa uchaguzi huo atatwikwa jukumu la kuiongoza Senegal, inayotazamwa kama kinara wa demokrasia katika eneo la Afrika Magharibi lililokumbwa na matukio ya mapinduzi, na kuiondoa katika matatizo yake ya karibuni na kusimamia mapato kutoka kwa hifadhi za mafuta na gesi ambazo zinatarajiwa kuanza uzalishaji hivi karibuni.
Sintofahamu ilitanda kuhusu matokeo ya uchaguzi huo, huku matokeo rasmi yakitarajiwa mwishoni mwa wiki na wingi mkubwa wa kura ukihitajika ili kumpata mshindi wa moja kwa moja katika duru ya kwanza.
Kiongozi wa upinzani Faye alikuwa amewaahidi wapiga kura mabadiliko makubwa na ya kweli. Na ameonekana kupata uongozi wa mapema dhidi ya aliyekuwa Waziri mkuu wa zamani wa muungano unaotawala Amadou Ba, kwa mujibu wa matokeo ya awali kutoka vituo vya kupigia kura yaliyochapishwa na vyombo vya habari vya nchini humo na kwenye mitandao ya kijamii.
Wagombea saba kati ya 17 wa urais wamempongeza Faye kutokana na dalili za mwanzo za kura zinazoendelea kuhesabiwa.
“Hongera kwa Bassirou Diomaye Faye kwa ushindi wake usio na shaka,” mgombea pekee mwanamke, Anta Babacar Ngom, aliandika kwenye mtandao wa X.
Dethie Fall alimpongeza Faye “kwa ushindi wake murwa, uliopatikana hasa kwa kuzingatia mienendo imara inayoibuka”.
Faye, mwenye umri wa miaka 44, na Ba (62) wote wakiwa wakaguzi wa zamani wa ushuru – waliibuka kuwa wagombea waliopigiwa upatu kushinda uchaguzi huo kati ya wagombea 17.
Mamia ya watu walikusanyika katika makao makuu ya kampeni ya Faye katika mji mkuu Dakar Jumapili usiku, wakiimba na kucheza ngoma.
Hali ilikuwa ya ukimya zaidi miongoni mwa wafuasi wachache waliokusanyika katika makao makuu ya kampeni ya Ba.
Ushindi kwa mpinzani Faye huenda ukaanzisha mabadiliko makubwa ya kimfumo nchini Senegal.
Leave a comment