SERIKALI ipo mbioni kuanza matumizi ya teknolojia ya kisasa katika shughuli za upakuaji mafuta kutoka kwenye meli ili kuepuka udanganyifu na upotevu wa mapato ya Serikali. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Katika utekelezaji wa mpango huo Serikali kupitia PBPA imekamilisha taratibu za ununuzi wa Mfumo wa Kusoma Mita Zote za Kupima Mafuta Wakati Wote (24/7).
Waziri wa Nishati, Januari Makamba, akiwasilisha hotuba ya bajeti leo Jumatatno tarehe 1 Juni amesema mfumo huo ujulikanao kwa jina la Supervisory Control and Data Acquisition (SCADA) utasoma mita zote zinazomilikiwa na Mamlaka ya Bandari Tanzania pamoja na mita zote zinazopima mafuta yanayoingia katika maghala ya Kampuni za Mafuta (OMCs).
Waziri huyo amesema kuwepo kwa mfumo huu kutawezesha ufuatiliaji “mubashara” wa upakuaji mafuta kutoka kwenye meli kwenda katika maghala ya mafuta na “kugundua/ kutahadharisha kwa haraka panapotokea ukiukwaji wa taratibu za upakuaji mafuta kutoka kwenye meli.
“Hivyo, mfumo huu utahakikisha kuwa mafuta yanapokelewa katika maghala yaliyokusudiwa kwa wakati wote,” amesema Makamba.
Amesema wakandarasi wa kutekeleza mradi huu wamepatikana na ufungaji wa mfumo huo unatarajiwa kukamilika mwezi Mei, 2023.
Katika hatua nyingine Makamba amesema Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA) ipo katika mpango wa maboresho ya miundombinu ya kuhudumia meli na shehena zote ikijumuisha bidhaa za mafuta ya petroli.
Amesema katika mpango wa muda mfupi TPA inakamilisha ununuzi wa mkandarasi atakayefanya kazi ya ukarabati wa gati la kupokelea mafuta la Kurasini (KOJ) katika robo ya kwanza ya mwaka wa fedha 2022/2023.
Kwa upande wa mpango wa muda mrefu, amesema TPA inatarajia kukamilisha Upembuzi Yakinifu na Tathmini ya Athari kwa Mazingira ya mradi wa ujenzi wa kituo cha kupokelea mafuta katika Bandari ya Dar es Salaam kabla ya kumalizika kwa mwaka 2021/22.
“Utekelezaji wa mpango huu utaongeza uwezo wa miundombinu ya bandari wa kupokea mafuta mengi kwa wakati mmoja,” amesema Makamba.
Leave a comment