WAFANYABIASHARA pamoja na watuaji wa nguo za mitumba nchini Kenya, wameitaka serikali nchi hiyo kusitisha mpango wake wa kupiga marufuku wa uingizwaji wa nguo hizo nchini humo. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa…(endelea).
Serikali ya Kenya imesema inataka kutumia malighafi yake kutengeneza nguo zake nchini humo ili kuunda ajira za Wakenya.
Katika masoko mbalimbali nchini Kenya, biashara ya nguo ya mitumba inadaiwa kushika kasi huku watu wengi wenye kipato cha chini wakitajwa kutegemea nguo hizi kwa sababu unafuu.
Hata hivyo, Waziri wa biashara nchini Kenya, Moses Kuria alisema wameandaa mpango wa kupiga marufuku nguo hizo ili kuruhusu zile zinazotengenezwa nchini Kenya.
‘‘Si kila mtu anayevaa mitumba anataka kuvaa, ni kwa sababu hana namna, ninataka kuona Kenya ambayo kila Mkenya anamudu kuvaa nguo mpya,” alisema waziri huyo.
Kwa mujibu wa wafanyabiashara na watumiaji wa nguo hizo, hatua hiyo itadumaza biashara hiyo inayotegemewa na mamilioni ya watu.
“Serikali inatakiwa itusikilize sisi watu wa chini kwa sababu tunahangaika sana.” alisema mmoja wa wauzaji wa nguo za mitumba nchini Kenya.
Hata hivyo, Chama cha Wafanyabiashara wa nguo za Mitumba nchini Kenya, kimehimiza serikali kupiga jeki biashara hiyo badala ya kuipiga marufuku.
“Kila wakati waauzaji wa nguo za mitumba wanaposikia biashara hiyo inafungwa huwa tunajiona kama wakimbizi katika nchi yetu.” alisema mmoaj wa viongozi wa chama cha wafanyibiashara wa nguo hizo.
Mitumba inachangia takriban ajira milioni 3.4 Afrika Mashariki.
Aidha, sekta hiyo ilisaidia Serikali za nchi wanachama wa Afrika Mashariki kupata mapato ya yaliyokadiriwa kuwa dola za Marekani milioni 419 mwaka 2021 kupitia kodi ya matumizi na mapato yanayohusiana na nguo za mitumba.
Leave a comment