MAHAKAMA Kuu, Kanda ya Mbeya Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya leo Alhamisi imetupilia mbali kesi ya kikatiba iliyofunguliwa na wananchi wanne wakiongozwa na Wakili Boniface Mwabukusi na wenzake iliyokuwa vifungu vya mkataba wa ushirikiano wa kiuchumi kati ya Serikali ya Tanzania na Dubai ikiwamo kwenye uwekezaji bandari za Tanzania kupitia kampuni ya DP World. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mbeya … (endelea).
Kesi hiyo namba 05/2023 iliwahusisha Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Dk. Eliezer Feleshi; Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa; Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi na Katibu wa Bunge, Nenelwa Mwihambi.
Katika hukumu iliyosomwa leo tarehe 10 Agosti 2023 na jopo la Majaji wa Mahakama Kuu, Masjala Kuu, mahakama hiyo imedai mkataba huo haukukiuka vifungu vya Katiba wala sheria za nchi.
Jopo la Majaji wa Mahakama Kuu, Masjala Kuu, Dustan Ndunguru, Mustafa Ismaili na Abdi Kagomba limeketi na kutoa hukumu kuhusiana na kesi hiyo iliyofunguliwa na waombaji wane tarehe 3 Julai 2023.
Waombaji hao walikuwa ni Alphonce Lusako, Emmanuel Kalikenya Chengula, Raphael Japhet Ngonde, na Frank John Nyalusi.
Malalamiko hayo waliyawasilisha kama kesi ya kikatiba na yaliwasilishwa dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi na Katibu wa Bunge.
Kwa mujibu wa taarifa kuhusu hukumu hiyo iliyotolwa kwa wanahabari na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Projestus Kahyoza imefafanua kuwa mahakama ilieleza kuwa, katika usikilizaji wa shauri hilo, uliochukua takribani siku tatu, Mahakama ilizingatia au kutoa majibu kwa kuangalia vini vikubwa sita.
Taarifa hiyo imefafanua viiini hivyo kuwa endapo utiaji saini, uwasilishaji na uridhiaji wa mkataba wa IGA ulikiuka matakwa ya kifungu cha 11 (1) and (2) cha Sheria ya Utajiri wa Maliasili asilia, Namba 5 ya mwaka 2017, kikisomwa kwa pamoja na viungu vya 5 (1), 6 (2) (a) (b). (e) na (1) vya Sheria ya mapitio na majadiliano ya vifungu visivyo vya haki vya mikataba ya utajiri wa maliasili asilia namba 6 ya 2017.
“Endapo umma ulijulishwa ipasavyo na kupewa fursa ya kushiriki kwenye mjadala na kutoa maoni kwa mujibu wa sheria katika mchakato wa kuridhiva kwa IGA; Endapo lbara za 2, (2) 5 (4), 6 (2), 7 (2), 8 (1) (a) (b) (C) 8, (2) 10 (1), 20 (2) (a) (e) () & (), 18, 21, 23 (1) na lbara za 26, 27 na 30 za lGA zinakiuka ibara za 1, 8, 28 (4) & (3) za Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
“Endapo IGA ni Mkataba; Endapo Ibara za 2 na 23 za IGA zimekiuka kifungu cha 25 cha Sheria za Mikataba; na endapo mkataba wa IGA kati ya URT na Dubai ulifuata utaratibu wa kisheria na mfumo wa manunuzi uliobainishwa katika kifungu cha 64 cha Sheria ya Nanunuzi ya Umma,” imesema taarifa hiyo.
Imeongeza kuwa viini hivyo vililenga kuhoji kama mkataba wa IGA ulikiuka vifungu vya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania na sheria ya Mikataba, Manunuzi ya Umma na Sheria ya Utajiri wa Maliasili asilia, Namba 5 ya mwaka 2017, Sheria ya Mapitio na Majadiliano ya vifungu visivyo vya haki ya mikataba ya Utajiri wa Maliasili asilia Namba 6 ya 2017.
Aidha, katika hukumu yake, Mahakama imebaini na kuhitimisha kuwa Mkataba wa IGA haukukiuka vifungu ya Katiba au sheria mbalimbali zilizonukuliwa hapo juu.
Aidha, imesema mahakama imetupilia mbali hoja za upande wa Waleta Maombi kwamba Mkataba wa IGA ulipoka uhuru wa Tanzania kumiliki na kutumia rasilimali asilia bila kuingiliwa na nchi yoyote.
“Vile vile, Mahakama haikuona kama usalama wa nchi ulikuwa hatarini kutokana na kusainiwa kwa Mkataba wa IGA. Kwa msingi huo, Mahakama imetupilia mbali shauri hilo na kuamuru kuwa kila upande ubebe gharama zake za kesi,” imesema taarifa hiyo.
Leave a comment