RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Pombe Magufuli amemteua, Kassim Majaliwa kuwa Waziri Mkuu wa nchi hiyo kwa kipindi cha miaka mitano ijayo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Jina la Majaliwa, limewasilishwa bungeni leo Alhamisi tarehe 12 Novemba 2020 jijini Dodoma na mpambe wa Rais Magufuli ili kuthibitishwa na Bunge hilo kwa mujibu wa Katiba ya Tanzania.
Shughuli za Bunge zilianza leo asubuhi ambapo, Spika Job Ndugai alimwapisha Rose Tweve wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kisha akatangaza kuahirisha kwa nusu saa shughuli za Bunge.
“Ninaahirisha shughuli za Bunge kwa muda wa nusu saa, tujiandae. Humu ndani kila mmoja ana fursa isipokuwa mimi,” alisema Spika Ndugai.
Gari la mpambe wa Rais Magufuli liliwasili viwanja vya Bunge saa 3:44 asubuhi akiwa amelibeba jina hilo la waziri mkuu mteule.
Bunge lilirejea na Spika wa Ndugai alimwita mpambe wa Rais kuingia bungeni ili kuwasilisha jina hilo ikiwa ni saa 3:53 asubuhi.
Spika Ndugai amesema, bahasha ina mihuri sita ya siri na baadaye ilifunguliwa na katibu wa bunge.
“Barua hii imetoka kwa Rais wa Jamhuri Muungano wa Tanzania, ikielekezwa kwangu ikihusu uteuzi wa waziri mkuu wa Tanzania,” amesema Spika Ndugai
Spika Ndugai alilitaja jina la waziri mkuu mteule aliyeteuliwa na Rais John Pombe Magufuli “nimemteua Kassim Majaliwa kuwa waziri mkuu.”
Baada ya Spika Ndugai kulitaja jina hilo la Majaliwa, shangwe ziliibuka bungeni kwa baadhi ya wabunge kwenda alipokuwa amekaa Majaliwa na kumpongeza.
“CCM, CCM, CCM…! Ziliendelea shangwe hizo bungeni huku Spika Ndugai amuwaomba wabunge waliokuwa wamekwenda kumpongeza kumpisha ili asogee mbele kwani alikuwa amekaa viti vya nyuma.
Baada ya shangwe hizo, Spika Ndugai ameahirisha kwa muda shughuli za Bunge ili kumpa nafasi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Profesa Adelardus Kilangi kuandaa wasifu wa waziri mkuu huyo mteule.
Kisha baadaye, Katibu wa Bunge, Stephen wa Bunge aliomba shughuli zisitishwe ili kuandaa azimio la Bunge la kumthibitisha Majaliwa kuwa waziri mkuu na karatasi za kura ili upigaji kura ufanyike.
Endapo, Majaliwa atathibitishwa na Bunge, kuendelea na wadhifa huo baada ya kumaliza muhala wa kwanza wa miaka mitano tarehe 5 Novemba 2020, atakuwa waziri mkuu wa kumi.
Majaliwa aliyezaliwa tarehe 22 Desemba 1961 ambaye kitaaluma ni mwalimu, atahudumu nafasi hiyo kwa miaka mitano hadi 2025 akiwa waziri mkuu wa kumi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Majaliwa aliingia bungeni kwa mara ya kwanza mwaka 2010 baada ya wananchi wa Jimbo la Ruangwa Mkoa wa Lindi walipomchagua katika uchaguzi mkuu wa wakati huo.
Rais wa wakati huo, Jakaya Mrisho Kikwete, alimteua kuwa naibu waziri, ofisi ya waziri mkuu-tawala za mikoa na serikali za mitaa (Tamisemi) kuanzia 2010-2015.
Mara baada ya uchaguzi mkuu kumalizika wa mwaka 2015 na Dk. Magufuli kuapishwa kuwa Rais wa Tanzania tarehe 5 Novemba 2015, alifanya uteuzi wa waziri mkuu.
Uteuzi huo ulifanyika tarehe 19 Novemba 2015 na kuliwasilisha bungeni ambapo lilithibitishwa akichukua nafasi iliyoachwa wazi na Mizengo Pinda.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI TV, MwanaHALISI Online na mitandao yetu kwa taarifa na habari mbalimbali
Leave a comment