AJALI mbaya imetokea usiku wa kuamkia leo Jumamosi, tarehe 13 Novemba, 2021 katika maeneo ya Mbezi kwa Yusufu, Dar es Salaam baada ya magari matano kugongana. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea)
Kwa mujibu wa Mkuu wa usalama barabarani wilaya – Kimara (DTO), Inspekta Adriano amesema ajali hiyo imetokana na uzembe wa madereva.
Amesema ajali ya kwanza ilitokea muda wa saa tano usiku jana tarehe 12 Novemba, 2021 baada ya dereva wa gari ndogo aina ya Land Cruiser mali ya Benki ya CRD iliyokuwa inatokea barabara ndogo kuingia barabara kuu bila tahadhari ya kulipisha gari ya mizigo (Mitsubishi Canter) lililokuwa likitokea Dar es Salaam kuelekea mkoani Iringa.
Amesema Canter hilo liliigonga gari hiyo ndogo na kuanguka barabarani.
Aidha, baadaye muda wa saa nane usiku lori jingine ambalo lilikuwa likitokea Kibaha mkoani Pwani kuelekea Dar es Salaam ambapo dereva wake hakufahamu kama mbele yake kuna ajali, aliligonga Canter hilo lililokuwa limeanguka na kuharibika vibaya.
Muda mfupi baadaye kutokana na kadhia katika eneo hilo la ajali, magari mengine mawili aina ya Toyota Noah na Toyota IST nayo yaligongana na kuharibika vibaya.
Aidha, dereva wa canter iililoanguka katika ajali ya kwanza aliumia mkono wa kulia na kukimbizwa katika hospitali ya Mloganzila.
Leave a comment