MWANAHARAKATI na mmiliki wa chaneli ya Ishema TV katika mtandao wa Youtube, Dieudonné Niyonsenga amehukumiwa kwenda jela miaka saba na kulipa faini Euro 4,280 (Sh milioni 11.2) baada ya kupatikana na hatia ya kutumia chaneli yake kuikosoa Serikali ya Rwanda. Anatipoti Mwandishi Wetu … (endelea)
Niyonsenga ambaye ni raia wa Rwanda na maarufu kwa jina la Cyuma kwa Kinyarwanda au chuma kwa Kiswahili, alipata watazamaji zaidi ya milioni 15 kwenye chaneli yake wakati akilaani ukiukwaji wa haki za biandamu nchini humo.
Licha ya kutokuwepo mahakamani, Alhamisi tarehe 11 Novemba mwaka huu, Mahakama nchini humo, ilimkuta na hatia ya makosa manne, ikiwa ni pamoja na kughushi na wizi wa utambulisho.
“Mahakama inazingatia kwamba makosa ambayo Niyonsenga anashtakiwa yalitekelezwa kwa makusudi.
“Mahakama inaamuru Dieudonné Niyonsenga akamatwe mara moja na kupelekwa kutumikia kifungo chake gerezani,” amesema Jaji wakati akitoa uamuzi huo.
Hata hivyo, Wakili wa Chuma, Gatera Gashabana amewaeleza waandishi wa habari kuwa anatarajia kukata rufaa juu ya uamuzi huo.
Nyota huyo wa YouTube hakufika mahakamani na alikamatwa nyumbani kwake muda mfupi baada ya kesi hiyo.
Chuma au Dieudonné Niyonsenga alikamatwa jana tarehe 12 Novemba mwaka huu ikiwa ni utekelezaji wa uamuzi wa mahakama.
Msemaji wa polisi nchini Rwanda, Thiery Murangira amelieleza Shirika la Habari la AFP kuwa sasa Chuma anajiaandaa kufikishwa jela kutumikia kifungo chake.
Hii ni mara ya pili kukumbwa na hatia kwani Aprili mwaka 2020, alichapisha mtandaoni video zilizowashutumu wanajeshi wa Rwanda kwa unyanyasaji dhidi ya wakazi wa makazi duni ambao walizuiliwa kutoka nje kama moja ya masharti ya kupambana na janga la corona.
Muda mfupi baadaye, alikamatwa na kushtakiwa kwa kukiuka hatua za kizuizi kwa kujifanya mwandishi wa habari, kabla ya kupelekwa gerezani.
Alifutiwa mashitaka na kuachiliwa miezi 11 baadaye, lakini waendesha mashtaka walikata rufaa.
Leave a comment