KATIBU Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad amesihi Rais John Magufuli aitishe kikao cha dharura kitakachoshirikisha watendaji mahsusi wa kiserikali pamoja na viongozi wa dini na kisiasa ili kujadili namna ya kukabiliana na vitendo vya ukatili na uvunjifu wa amani vinavyoendelea kujitokeza nchini, anaandika Mwandishi wetu.
Maalim Seif amesema ameamua kutoa nasaha hiyo akirejea tukio la kujeruhiwa kwa risasi nyingi Mnadhimu Mkuu wa Kambi rasmi ya Upinzani nchini, Tundu Lissu ambaye bado anatibiwa katika Hospitali ya Agha Khan, jijini Nairobi, baada ya kushambuliwa na watu wanaosadikiwa kuazimia kumtoa roho.
Lissu ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki na Mwanasheria Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), alipigwa risasi Septemba 7, mchana mjini Dodoma, wakati akiwasili nyumbani kwake Area D, akitokea bungeni.
Maalim Seif alikuwa akifungua Mkutano Mkuu wa Jumuiya ya Vijana wa CUF (JUVICUF) wa Wilaya ya Kaskazini ‘A’ Unguja jana. Amesema shambulio dhidi ya kiongozi wa ngazi ya kitaifa kama Lissu, limemshtua moyo kwa kuwa haikutarajiwa wawepo watu wenye moyo wa ukatili kiasi hicho.
Amesema ni kitendo kinachoonesha katika nchi kwa sasa kuna tatizo kubwa la kijamii ambalo linasababisha hata usalama wa raia na mali zao kuwa usiotabirika.
“Si kitendo kizuri hata kidogo. Binafsi kimenishtua moyoni kwamba kinamtokezea kiongozi wa ngazi ya kitaifa kama Lissu… tunalo tatizo na naona kuna haja ya serikali ya Jamhuri ya Muunganowa Tanzania kuitisha kikao kitakachoshirikisha viongozi wa dini ya kisiasa kujadili na kupata njia nzuri itakayosaidia kuepusha matukio mabaya namna hii,” alisema.
Amesema kitendo kilichofanywa na kwa kupima matukio kadhaa ya uvunjaji wa haki za binaadamu ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kinaashiria ni kwa kiasi gani nchi inakabiliwa na uvunjaji wa misingi ya haki za binaadamu.
“Ninalaani vikali kitendo hichi na kulitaka Jeshi la Polisi kuwatafuta watu waliohusika nacho ili wachukuliwe hatua kwa mujibu wa sheria za nchi yetu… tena uchunguzi ufanywe kisayansi na matokeo yake yatangazwe kwa wakati muafaka,” alisema.
Inspekta Jenerali wa Polisi Simon Sirro ametangaza kuwa upelelezi umeanza baada ya kupeleka timu ya makachero hodari kutoka Makao Makuu ya Polisi nchini. Ametaka mtu yeyote mwenye taarifa zitakazosaidia upelelezi huo kuziwasilisha polisi.
Leave a comment