MBUNGE Viti Maalumu asiye na chama bungeni, Anatropia Theonest, amehoji Serikali ina mpango gani wa kutatua changamoto ya upungufu wa vituo vya afya na zahanati, katika Wilaya ya Kyerwa mkoani Kagera. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Anatropita amehoji hayo leo Jumanne, tarehe 15 Juni 2021, katika kipindi cha maswali na majibu, bungeni jijini.
Kwa mujibu wa Anatropita, wilaya hiyo ina upungufu wa vituo vya afya 21, kwa kuwa idadi iliyopo sasa ni tatu katika kata 24, huku upungufu wa zahanati ukiwa 76. Kinyume na matakwa ya sera ya afya, inayoelekeza kila kata kuwa na kituo cha afya.
“Kwa kuwa ni sera ya Serikali kuwa na zahanati kwa kila kijiji, lakini kituo cha afya kwa kila kata. Kyerwa yenye kata 24 ina zahanati tatu. Ina vijiji 99 lakini ina zahanati 23. Ningependa kujua kwa wilaya hiyo, sera inatekelezwaje?” Amesema Anatropita.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri Ofisi ya Rais-Tamisemi, Dk. Festo Dugange, amesema Serikali inaendelea kutekeleza sera hiyo kwa kujenga vituo vya afya na zahanati maeneo mbalimbali nchini.
Na kwamba katika kipindi cha miaka mitano (2015/16 hadi 2020/21), imejenga zahanati 1,281 na vituo vya afya 488 na hospitali za halmashauri 102.
Amesema, mkakati huo unaendelea kutekelezwa , huku akihidi kwamba Wilaya ya Kyerwa itapewa kipaumbele kwenye awamu inayofuata.
“Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/22, Serikali itaendelea na ujenzi wa vituo vya afya 121 na kiasi cha Shilingi billioni 27.75 kimetengwa kwa ajili ya umaliziaji wa maboma768, ya zahanati kote nchini,” amesema Dk. Dugange.
Leave a comment