Baada ya kuibuka na ushindi finyu wa bao 1-0 dhidi ya Biashara United kocha wa klabu ya Yanga Boniface Mkwasa amesema kuwa kitendo cha wachezaji wake kusafiri kwa muda katika michezo ya Ligi kuu na bila kupata nafasi ya kupumzika kimefanya timu yake kucheza chini ya kiwango kwenye mchezo wa leo wa Ligi Kuu. Anaripoti Kelvin Mwaipungu… (endelea)
Mkwasa amesema kuwa pamoja na kuibuka na ushindi huo lakini hakuridhishwa na kiwango kilichooneshwa na timu yake katika mchezo kutokana na ratiba ilivyo kwenye michezo ya Ligi Kuu.
“Tumerudi juzi tu na kushinda jana ndio maana unaona kuna uchovu na baadhi yao unaona miili yao inakakataa, lakini yote kwa yote tumepata ushindi na kuibuka na alama tatu licha ya kupoteza nafasi nyingi kipindi cha kwanza” alisema Mkwasa
Mkwasa aliongezea kuwa timu ya Biashara ni nzuri na kama itacheza hivi katika michezo yote basi inaweza kupata matokeo lakini wachezaji wake walipambana licha ya kuwa katika mazingira magumu.
Yanga ambayo imecheza michezo mitatu ya Ligi ndani ya siku saba ambayo miwili kati ya hiyo wamecheza kanda ya ziwa dhidi ya Mbeya City kwenye uwanja wa Sokoine Mbeya na kutoka sare, huku mchezo mwengine ukiwa dhidi ya Tanzania Prisons uliochezwa Iringa kwenye Uwanja wa Samora na kufanikiwa kuibuka na ushindi wa bao 1-0.
Bao la Yanga kwenye mchezo wa leo limefungwa na mshambuliaji wao mpya Tariq Seif kwenye dakika ya 85, ikiwa ni mechi yake ya kwanza baada ya kusajiliwa kwenye dirisha dogo la usajiri hivi karibuni.
Baada ya ushindi huo yanga inafikisha jumla ya alama 24 na kushika nafasi ya pili kwenye msimamo nyuma ya Simba ambayo ina alama 31 baada ya kucheza michezo 13 huku wote wawili hao wakitarajia kukutana kwenye mchezo ujao wa Ligi Kuu utakaochezwa tarehen 4, januari 2020 kwenye uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Leave a comment