KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida mwanamke aliyefahamika kwa jina la Veronica Paul (27) amedaiwa kumuua kikatili mtoto wa kambo Mageshi Busanda (7) kwa kumcharaza kwa bakora na kumkanyaga kifuaji kisha kumtupa porini.
Mwanamke huyo anadaiwa kutenda unyama huo baada mtoto huyo kudaiqa kupoteza ng’ombe wawili. Anaripoti Ibrahim Yassin…(endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari leo tarehe 6 Julai 2023, Kamanda wa polisi mkoani Songwe, Theopista Mallya amesema tukio hilo limetokea katika kitongoji cha Katavi ‘A’ kijiji na kata ya Gua wilayani Songwe mkoani hapa.
Amesema Nobhanilo Busanda ambaye pia ni mkazi wa kijiji hicho ndiye mwenye mtoto huyo aligundua mwanae kuuawa na mama huyo wa kambo na kutoa taarifa polisi iliyofanikisha kukamatwa kwake.
Amesema baada ya mama huyo wa kambo kukamatwa leo muda wa asubuhi na kuhojiwa, alikiri kutekeleza mauaji hayo na kuelezea namna alivyofanya ukatili huo.
Amesema alitekeleza mauaji hayo baada ya mtoto huyo kupoteza ng’ombe wawili, tarehe 28 Juni 2023 kisha alimuadhibu kwa kumpiga na fimbo maeneo mbalimbali ya mwili wake kisha kumkanyaga kifuani na kumsababishia mauti.
Amesema baada ya kutekeleza mauaji hayo, alimtupa porini umbali wa mita 355 kutoka nyumbani kwake.
Kamanda Mallya ameendelea kufafanua kuwa shauri lake limefikishwa mahakamani kwa hatua zaidi za kisheria.
Aidha, amewataka wananchi kushirikiana na jeshi la polisi kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu ili wachukuliwe hatua na kutokomeza matukio hayo katika mkoa wa Songwe.
Leave a comment