MKURUGENZI wa Habari, Uenezi, Mahusiano na Umma wa Chama cha Wananchi (CUF) nchini Tanzania, Mhandisi Mohamed Ngulangwa na wenzake watano, wamefutiwa kesi ya uhujumu uchumi, iliyokuwa inawakabili katika Mahakama Kuu Iringa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Iringa … (endelea).
Kesi hiyo ya uhujumu uchumi Na. 6 iliyofunguliwa na Serikali mwaka 2018, imefutwa leo Jumanne, tarehe 12 Oktoba 2021, mbele ya hakimu aliyepewa mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo, Hakimu Mkazi, Respicius Mwaijage.
Kesi hiyo ilifutwa mbele ya mahakama hiyo, baada ya upande wa Jamhuri kuieleza kwamba haina nia ya kuendelea nayo na kuomba ifutwe.
Awali, kesi hiyo ilidumu kwa miaka mitatu bila kusikilizwa na au upelelezi wake kukamilika.
Mbali na Mhandisi Ngulangwa, wengine waliokuwa wameshtakiwa kwa kesi hiyo ni, Mhandisi Godwin Mshana, ambaye ni mmiliki wa Kampuni ya Ujenzi ya MNM Engineering Service Limited. Prof. Philemon Mushi, aliyekuwa Mkuu wa Chuo cha Mkwawa kuanzia 2007 hadi 2012.
Wengine ni, Prof. John Machiwa, aliyekuwa Makamu Mkuu wa chuo hicho, kitengo cha utawala (2009-2012) na Jackson Matandu, Mjumbe wa Bodi ya Zabuni.
Ngulangwa ambaye kwa sasa ni mkurugenzi wa Habari CUF, alidaiwa kutenda kosa hilo akiwa Meneja Miliki na Mjumbe wa Bodi ya Zabuni ya Chuo Kikuu cha Mkwawa.
Ngulangwa na wenzake walifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza Juni 2018, wakikabiliwa na mashtaka ya kuisababishia hasara Serikali ya Sh. 2.4 bilioni, alizolipwa mkandarasi MNM Engineering Service Limited, katika mradi wa ujenzi wa ukumbi wa mihadhara wa Chuo Kikuu cha Mkwawa mkoani Iringa.
Hata hivyo, Ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), ya ukaguzi maalum ya 2018, ilibainisha kwamba hakuna Fedha iliyopotea kwenye mradi huo na kwamba mkandarasi huyo alikuwa amelipwa pungufu ya fedha aliyostahili kulipwa, mpaka aliposimamishwa kazi Julai 2017.
Hongereni sana