MWENYEKITI wa Bodi ya Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Stephen Wasira amemuelezea Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere alikuwa kiongozi aliyekuwa mstari wa mbele kwa ajili ya kutetea maslahi ya Watanzania. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Wasira ambaye ni waziri mwandamizi aliyehudumu serikali ya Mwalimu Nyerere, Hayati Benjamin Mkapa amesema, Mwalimu Nyerere alikemea udini, ukabila na aliamini kuwa binadamu wote ni ndugu.
Amesema hayo leo Jumanne, tarehe 12 Oktoba 2021, kwenye kongamano la Kumbukizi ya miaka 22 ya Kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu, Julius Nyerere, katika Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Kivukoni jijini Dar es Salaam.
Mwalimu Nyerere alifikwa n amauti tarehe 14 Oktoba 1999, London nchini Uingereza alikokwenda kwa matibabu na mwili wake ulizikwa Butiama, mkoani Mara.
“Baba wa Taifa aliamini katika umoja, usawa na utu na ndiyo maana hata ukiangalia mada kuu ambayo inajadiliwa katika kongamano hilo inasema, Maono ya Mwalimu Nyerere katika uongozi, maadili, umoja na amani kwa maendeleo ya jamii.
Awali, Mkuu wa chuo hicho, Profesa Shadrack Mwakalila alisema chuo kinatoa mafunzo ya uongozi, maadili, uzalendo pamoja na kunafanya tafiti ambazo zinatatua changamoto katika jamii.
Alisema, kinatoa ushauri kwa sekta binafsi, kinatoa na pia kozi ambazo zinakidhi mahitaji ya kila ngazi kuanzia kijiji, wilaya, mkoa na Taifa.
Profesa Mwakalila alisema chuo kila mwaka kimekuwa kinaadhimisha makongamano matatu ambayo lengo la makongamano hayo ni sehemu ya kuwaenzi waasisi wa Taifa ambao ni Hayati Mwalimu J. K. Nyerere na Sheikh Abeid Karume.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Mzee Joseph Butiku alisema Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere aliamini watu wote ni sawa na haki zote ni sawa hivyo lazima kila mmoja aheshimu utu wa kila mtu.
Leave a comment