MCHUNGAJI wa Kanisa la Calvary Assemblies of God ameiangukia Serikali na kuiomba iwasaidie kudhibiti watu wenye nia ovu ya kutaka kuondolewa kwa kanisa hilo lililoko eneo la Ubungo Maziwa jijini Dar es Salaam. Anaripoti Juliana Assenga UDSM … (endelea)
Akizungumza katika ibada ya Jumapili jana mchungaji wa kanisa hilo Imelda Maboya alisema ameshangazwa na uvamizi uliofanyika kanisani hapo licha ya kuwepo katika eneo hilo kwa zaidi ya miaka 22.
Alisema kanisa hilo lipo eneo la Tanzania Steal Pipe (TSP) ambalo walikabidhiwa kipindi cha ubinafsishaji na kupewa ofa maalumu ambayo ilitolewa kipindi cha ubinafsishaji wa mashirika ya umma (PCRC), ambapo walielezwa kwamba wangepewa kipaumbele endapo ikitokea pakauzwa.
“Mahali hapa lilipo kanisa kulikuwa ni kichaka cha wavuta bangi, walevi na wahuni wengine, kanisa limesaidia kuiondosha hali hiyo,” alisema.
Ameiomba serikali kuanzia wilaya, mkoa na Taifa kuwasaidia ili kuliweka sawa suala hilo.
Muumini Sylvia Rweyemamu ameliomba Rais kusikia kilio chao kwani mbali na ibada wanajipanga kutoa elimu kwa vijana kuhusiana na ‘panya road’ ambalo ndilo janga nchini.
Anna Nderumaki alishangazwa na uvamizi wa watu zaidi ya 100 waliovamia kanisani hapo kwa sababu katika maisha yake hajawahi kuona uvamizi kwenye nyumba ya ibada.
Ezron Matowo alimshukuru Rais kwa usikivu na huruma yake, na kusema suala kama hilo ni dogo kwake kwa sababu anayoyatekeleza yanaonekana.
Muumini Placid Malaki alitumia fursa hiyo kuiomba serikali kuwaongezea eneo kwa ajili ya kufanya ibada kwani wanachotekeleza kwa ajili ya nchi ni kikubwa zaidi.
Leave a comment