MCHUNGAJI Ambilikile Mwasapile (86), maarufu kama Babu wa Loliondo, amefariki dunia kwa ugonjwa wa nimonia. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumamosi, tarehe 31 Julai 2021 na Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Raymond Mangwala, akizungumza na wanahabari, siku moja baada ya Mchungaji Ambilikile kufariki dunia, akiwa njiani kuelekea katika Kituo cha Afya cha Digodigo wilayani humo.
Mangwala amesema kuwa, Mchungaji Ambilikile alianza kuumwa siku tano zilizopita na madaktari walimgundua anasumbuliwa na ugonjwa wa Nimonia, ambapo alipatiwa sindano za masaa alizomaliza juzi Ijumaa.
“Mchungaji Ambilikile ameugua kuanzia siku tano nyuma zilizopita, ilikuwa anaonekana ana homa kali akapangiwa sindano za masaa. Baada ya kumpima, madaktari wa kituo cha Digodigo waligundua ana nimonia ingawaje sio Covid-19,” amesema Mangwala.
Mkuu huyo wa wilaya amesema, hali ya Mchungaji Ambilikile ilibadilika jana mchana, hali iliyopelekea wasaidizi wake kumkimbiza katika kituo cha afya.
“ilikuwa Nimonia kali inamsumbua, akachoma sindano za masaa alimaliza juzi, jana aliamka kama kawaida. Katika sala zake amesali na wasaidizi wake na majirani. Ilivyofika saa tisa mchana alikuwa hajisikii vizuri, akawa analalamika chembe ya moyo inamsumbua,” amesema Mangwala.
Mangwala ameongeza “likatafutwa gari likafika akatoka ndani kwa mguu mpaka akafika kwenye gari, akanza kutapika. Ikaonekana ametutoka wakati huo huo. Wao wakasema tumuwahishe kituo cha afya lakini alivyofika wakasema ameshatutoka, kufika saa 10.30 daktari alithibitisha amekufa.”
Mangwala amesema, taratibu za mazishi zinasubiri watoto na familia ya marehemu , kwa ajili ya kuamua kama atazikwa Arusha au mkoani Mbeya, ambako inasadikika alikotoka.
Mchungaji Ambilikile alijizolea umaarufu kuanzia 2011 hadi 2013, nchini Tanzania na nje ya nchi, kufuatia tiba yake ya mitishamba ya kusaidia watu wenye magonjwa sugu, iliyofahamika kama kikombe cha babu wa Loliondo.
RIP mchungaji
Lakini kwa nini asitumie kikombe chake cha uponyaji badala ya kuwategemea madaktari? Au kimepungua nguvu?