Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) ambae ni mdhamini Mkuu wa Ligi Kuu ya Soka ya Tanzania Bara, NBC Premiere League jana Jumapili imekabidhi zawadi ya pesa na tuzo kwa kocha bora wa ligi hiyo wa mwezi Februari, Miguel Gamond kutoka klabu ya Yanga. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Makabidhiano ya zawadi hizo yalifanyika muda mfupi kabla ya kuanza kwa mchezo baina ya Azam FC dhidi ya Yanga SC uliofanyika katika Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam, mchezo ambao ulikamilika kwa timu ya Azam FC kuibuka na ushindi wa goli 2 -1.
Katika tukio la makabidhiano ya zawadi hizo, ilishuhudiwa Mkuu wa Kitengo cha Masoko wa benki ya NBC, David Raymond akikabidhi tuzo pamoja na mfano wa hundi ya pesa yenye thamani ya Sh milioni moja kwa kocha Gamondi ikiwa ni muendelezo wa utaratibu wa mdhamini huyo kutoa tuzo kama hizo kwa wachezaji na makocha bora kwa kila mwezi.
Kwa upande wa wachezaji, kipa wa Coastal Union ya Tanga, Ley Matampi alitangazwa kuwa mshindi wa tuzo hiyo kwa mwezi Februari.
“Kimsingi ni kwamba sisi kama wadhamini wa ligi hii tunaendelea kujivunia sana kuona ligi yenye ushindani na viwango bora vya kiuchezaji vinavyoendelea kuonekana kwenye ligi hii.
“Ndio maana utaona kwamba pamoja na ligi kuwa na wachezaji wengi wa kigeni bado wachezaji wazawa wanapambana na kufanya vizuri na wanachukua tuzo hizi. Huu ni uthibitisho kwamba vilabu vyote kwasasa vinaweza kuhudumia vyema wachezaji wake kiasi cha kuweza kutoa ushindani unaotakiwa,’’ alisema Raymond
Kwa mujibu wa Raymond, benki hiyo inaendelea na mikakati mbalimbali kuhakikisha timu hizo zinanufaika zaidi na udhamini wa benki hiyo kwenye ligi hiyo ambayo hadi sasa imetoa ajira na kipato kwa watu zaidi ya 12,000.
Aliitaja mikakati mbalimbali ikiwemo mikopo ya mabasi kwa vilabu mbalimbali vinavyoshiriki ligi hiyo ili kurahisha usafiri kwa vilabu hivyo, mpango ambao unahusisha hatua kadhaa hadi kufikia hatua ya kukabidhi aina hiyo ya usafiri.
“Na jitihada zetu hizi haziishii kwenye mchezo wa soka tu bali pia michezo mingine ikiwemo golf na mchezo wa riadha ambapo hivi karibuni tutazindua msimu wa mwaka huu wa NBC Dodoma Marathon inayofanyika kila mwaka jijini Dodoma ambapo tumekuwa tukikusanya fedha kwa ajili ya elimu na matibabu ya saratani ya shingo ya kizazi changamoto ambayo inachangia kwa kiasi kikubwa vifo vya kina mama.’’ alisema.
Leave a comment