MLIPUKO wa Virusi vya Ebola, umeibuka tena Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC). Inaripoti Mitandao ya Kimataifa…(endelea).
Taarifa ya mlipuko huo, imetolewa na wizara ya afya nchini humo, ambapo inaeleza mtu mmoja kutoka Mji wa Biena karibu na mji wa Butembo Jimbo la Kivu Kaskazini, amefariki dunia kutokana na virusi hivyo.
Taarifa ya wizara hiyo inasema, inapeleka timu ya wataalamu katika eneo hilo lenye mlipuko.
Jana Jumapili tarehe 7 Februari 2021, Umoja wa Mataifa (UN) , ulisema hadi saa watu 70 wamebainika walikuwa karibu na wagonjwa wa Ebola katika eneo hilo.
“Zaidi ya watu 70 wametambuliwa kuwa walikuwa na makaribiano na mgonjwa huyo aliyefariki dunia na kazi ya kutakasa maeneo aliyokuwa ametembelea inaendelea,” inaeleza taarifa ya UN.
Taarifa ya UN inasema, sampuli zilizochukuliwa kutoka kwa wagonjwa wawili ambao mmoja wake amefariki dunia, zimepelekwa maabara kuu ya Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa nchini DRC (INRB), ili kutambua aina ya virusi hivyo.
Naye Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Kanda ya Afrika, Dk. Matshidiso Moeti, amesema, shirika hilo linasaidiana na mamlaka husika kufanya uchunguzi, ili kubaini kutokomeza mlipuko wa Ebola.
Kwa mujibu wa mitandao ya kimataifa, mlipuko huo ni wa 12 kutokea nchini humo, ambapo mlipuko wa mwisho ulitokea Septemba 2020.
Leave a comment