AJALI za barabarani nchini Tanzania hasa kwa madereva wa pikipiki (bodaboda), zinasababishwa na adhabu kutoka kwa askari wa usalama barabarani (Trafiki). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa na Salome Makamba, Mbunge Viti Maalumu leo Jumatatu tarehe 8 Februari 2021, bungeni jijini Dodoma wakati akiuliza swali la nyongeza katika wizara ya mambo ya ndani.
Salome ni miongoni mwa wabunge 19 waliofukuzwa uanachama wa Chadema na Kamati Kuu (CC) ya chama hicho, kukiri kufukuzwa kwa kukata rufaa Baraza Kuu (BKT), na kuendele kuhudumu kwa wabunge kutokana na kukingiwa kifua na Spika wa Bunge, Job Ndugai
Akizungumza bungeni hapo, Salome amedai tatizo hilo linatokana na trafiki kukifanya kitengo cha usalama barabarani chanzo cha mapato.
Amedai, baadhi ya bodaboda hulazimika kuwakimbia ili kukwepa kutoa faini, hatimaye wengi wao kuangukia katika ajali.
“Tatizo la msingi la ajali za baraarani kwa bodaboda na vyombo vingine vya usafiri, linatokana na kitengo cha usalama barabarani kuwa kama chanzo cha mapato.”
“Watu wanakwepa ma-trafiki, wanakimbia sababu ukikamatwa, hakuna onyo ni faini,” amedai Salome
Amesema, tatizo la kukithiri kwa adhabu za makosa ya barabarani ni dosari zilizopo katika baadhi ya vifungu vya Sheria ya Usalama barabarani ya mwaka 1973.

“Bodaboda siku hizi wanakamatwa kwa kukimbiana na matrafiki, nadhani hii inasababishwa na uzee wa sheria ya mwaka 1973,” amesema Salome.
Akiuliza swali lake la nyongeza, Makamba amehoji lini serikali italeta muswada wa kufanya marekebisho ya sheria hiyo ili kupunguza ajali za barabarani.
“Serikali ni lini italeta mabadiliko ya sheria ya usalama barabarani ili tufungue mjadala wa kuboresha kupunguza ajali za baabarani?” amehoji Salome
Akijibu swali hilo, Khamis Hamza Chilo ambaye ni Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani amesema, muswada wa mabadiliko ya sheria hiyo uko njiani.
“Nimtoe hofu, muswada huu uko njiani, muda wowote tutaleta tuone namna tutafanya mabadiliko ya sheria hii,” amejibu Chilo.
Leave a comment