KUTOKANA na kukua kwa kasi ya Teknologia nchini na duniani kwa ujumla, Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI) kinatarajia kuboresha karakana ya mafunzo kwa kuongeza vifaa na maeneo ya kujifunzia ili kuendana na mabadaliko ya sayansi na teknolojia pamoja na soko la ajira. Anaripori Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Hayo yamesemwa jijini hapa leo tarehe 9 Februari 2023 na Kaimu Mkuu wa Chuo hicho, Dk. Tumaini Gurumo wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma kueleza utekelezaji wa majukumu wa taasisi hiyo.
Amesema ujenzi na ukarabati wa mifumo ya Tehama, itasaidia kutoa fursa ya mafunzo ya masafa marefu na kuzalisha mabaharia wenye kuendana na teknolojia za sasa.
Dk. Gurumo amesema maboresho hayo ya karakana yatasaidia wanafunzi wao kutokuwa wageni wa vifaa wanavyokutana navyo wanapokwenda kwenye mafunzo kwa vitendo.
Aidha, amesema DMI imeanza utaratibu wa kujenga uhusiano na wamiliki wa meli ili kupata nafasi za ajira na mafunzo kwa vitendo kwa ajili ya mabaharia wa kitanzania nje na ndani ya nchi.
“Tayari DMI imewaunganisha na waajiri mabaharia 27 na kupata ajira na mafunzo kwa vitendo,” amesema Dk. Gurumo.
Dk. Gurumo ameeleza kuwa Serikali imewezesha upatikanaji wa maeneo mbalimbali ya kujenga matawi ya DMI katika mikoa ya Lindi na Mwanza.
“Matawi hayo yatakapokamilika, huduma ya elimu na mafunzo ya usalama wa vyombo vya usafiri na usafirishaji kwa njia ya maji, itakuwa imesogezwa karibu zaidi na wananchi,” amesema.
Amesema matawi hayo yatawezesha vijana wengi zaidi kupata elimu na kupanua wigo wa ajira kwa sababu soko la ajira ya ubaharia nchini, linaendelea kuongezeka na katika ulimwengu ni kubwa kwa sasa.
Aidha, akizungumzia mipango mingine ya chuo hicho, amesema ni pamoja na kujenga vyombo vidogo vidogo vya usafiri majini ikiwa ni sehemu ya mafunzo kwa vitendo, kujenga miundombinu ya chuo kwa viwango vya juu mkabala na ufukwe wa bahari ya Hindi jijini Dar es Salaam ili kukidhi mahitaji ya ongezeko la wanafunzi, walimu na kozi.
Leave a comment