WAZIRI wa Fedha na Mipango nchini Tanzania, Dk. Mwigulu Nchemba, amefafanua jinsi kodi ya lini ya simu itakavyolipwa na watumiaji huku akiwaomba kujifunga mkanda ili kuijenga nchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Dk. Mwigulu, ametoa ufafanuzi huo leo Jumanne, tarehe 22 Juni 2021, bungeni jijini Dodoma, wakati akihitimisha mjadala wa Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2021/22 ya Sh.36.3 Trilioni.
“Jambo hili kwa kiwango fulani lilikuwa halijaeleweka, kwani wananchi walidhani makato haya yanakwenda kukatwa kila siku au usipoweka salio siku ukiweka inakatwa na ya jana, lahasha. Itakatwa pindi ukiweka salio.”
Amesema, wameangalia takwimu za watumiaji wote wa simu na viwango wanavyotumia kwa mwezi kisha wakapendekeza viwango tofauti tofauti za makato hayo kwa kila “mtu anapoongeza salio.”
“Wale watumiaji wanaotumia viwango vya chini Sh.1,000 kwenda chini, anakatwa Sh.5; anayetumia Sh.7,000 hadi 10,000 atakatwa Sh.75 na anayetumia Sh1,0000 hadi Sh.25,000 anakatwa Sh112. Kama anajiunga Sh.50,000 kwa mwezi mzima anakatwa Sh.186,” amesema Dk. Mwigulu
“Nilisema wakati nawasilisha bajeti kuwa nawahurumia Watanzania. Lakini kwa mtu anayetumia Sh.50,000 hivi kuchangia Sh.186, kuna ugumu gani kumchanghia mwanamke anayeteseka huko vijijini, nchi hii itajengwa na Watanzania wenyewe, lazima tubebe majukumu hayo kama wazazi, kama Watanzania kwa sababu majukumu hayo ni yetu,” amesema

Amesema, kiwango hicho cha fedha kitakachopatikana, kitakwenda kutatua changamoto mbalimbali ikiwemo ya maji “tutapunguza watoto wetu kubakwa na kuteseka, kutafuta maji. Shida ya maji bado ni tatizo katika maeneo mengi.”
Leave a comment