TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) leo Ijumaa, tarehe 20 Agosti 2021, inamfikisha Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa ya Temeke (DED), Lusubilo Mwakabibi kwa tuhuma mbalimbali ikiwemo matumizi mabaya ya madaraka. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Takukuru Mkoa wa Temeke imesema, Lusubilo atafikishwa mahakamani hapo asubuhi hii.
Tarehe 25 Aprili 2021, Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Ummy Mwalimu alitangaza kumsimamisha kazi Mwakabibi ili kupisha uchunguzi wa tuhuma zilizokuwa zinamkabili.
Waziri Ummy alisema, Mwakabibi anatuhumiwa kwa ubadhirifu na usimamizi usioridhisha wa miradi ya maendeleo katika halmashauri ya manispaa ya Temeke kutoka kwa wananchi, viongozi na vyanzo vingine.
Jumatatu ya tarehe 16 Agosti 2021, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alifanya ziara yake ya kikazi ya kukagua miradi ya ujenzi wa barabara za Kijichi-Mwanamtoti na Kijichi-Toangoma wilayani Temeke na kituo cha Mabasi kilichopo Buza. Mirado hiyo inajengwa kupitia mradi uendelezaji wa Jiji la Dar es Salaam (DMDP).
Katika ziara hiyo, Majaliwa hakuridhika na gharama za ujenzi wa miradi ya barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 1.8 iliyogharimu Sh.5.4 bilioni na barabara ya Kijichi-Toangoma yenye urefu wa kilomita 3.25 iliyogharimu Sh.13.5 bilioni.
Kufuatia hatua hiyo, Majaliwa aliagiza Taasisi za Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ihakikishe watu wote waliohusika na ubadhilifu huo wa fedha ambao tayari walishasimamishwa kazi wawe wamefikishwa mahakamani kabla ya 20 Agosti 2021.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI TV, MwanaHALISI Online na mitandao yetu ya kijamii kwa habari na taarifa mbalimbali.
Leave a comment