MKUU wa wilaya ya Ilala, Sophia Mjema ameagiza kuchukuliwa hatua askari wanaodaiwa kuwapiga wananchi katika eneo la Gongo la mboto Jijini Dar es Salaam kwa madai ya kulipiza kisasi, anaandika Hamis Mguta.
Mjema amesema hayo leo alipokuwa akizungumza na wananchi hao wa Gongo la mboto ambao kwa siku tatu mfululizo wamekuwa wakishambuliwa na askari kwa kile kinachoelezwa kuwa walikuwa wanalipiza kisasi baada ya askari mwenzao kukutwa ameuawa.
“Kama Mkuu wa wilaya na mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama jambo ambalo limefanyika kwa siku tatu hizo halikubaliki na kama kuna matatizo kati ya askari na raia kulikuwa kuna eneo la kupeleka matatizo hayo”
“Kama askari aliyekuwa amepatikana amefariki, utaratibu ilikuwa uchunguzi ufanyike ili kujiridhisha,” amesema Mjema.
Aidha, Mjema amesema wahusika wanatakiwa kuwachukulia hatua za kinidhamu askari waliofanya kitendo hicho.
“Askari walioshiriki kufanya jambo hili wachukuliwe hatua za kinidhamu na huko barabarani sitaki kumuona FFU yoyote anasumbua wananchi,” amesema.
Mmoja wa wananchi waliopigwa amesema tukio hilo lilitokea juzi saa mbili usiku ambapo askari hao walivamia maeneo mbalimbali, majumbani pamoja na maeneo ya biashara kisha kuanza kupiga watu.
Leave a comment