CHAMA cha Demokrasia ya Maendeleo (Chadema) kimefungua milango kwa watia nia wa urais wa chama hicho kuanzia leo Jumatano tarehe 3, Juni hadi Juni 15,2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari makao makuu wa Chadema, Katibu Mkuu chama hicho, John Mnyika amesema watia nia hao wataandika barua kwa katibu mkuu.
Amesema, baada ya hapo, atafikisha majina ya waliojitokeza kwa kamati kuu ambayo itayapitia,”tutatoa taarifa tena ya nini kitaendelea baada ya tarehe 15 Juni 2020.”
Pia, Mnyika amesema, chama hiko kimefungua milango ya majadiliano na vyama vingine vya siasa,”vyenye dhamira ya kuiondoa CCM madarakani, tutashirikiana nao.”
Kuhusu waliotia nia mapema kama alivyofanya Dk Myrose Majige ya kutangaza, amesema,”ili utie nia, lazima uandike barua kwa katibu mkuu, lakini kama umetia nia huko kwenye vyombo vya habari, mimi siwezi kuwazungumzia.
Mnyika amewataka watia nia wote kuhakikisha wanasoma vyema mwongozo wa chama hicho wa mwaka 2012 unaodhibiti rushwa ndani ya chama.
“Wagombea wanaotarajia kutia nia, wazingatie mwongozo na kama hawatofuata, chama hakitasita kuwachukulia hatua,” amesema Mnyika
Kuhusu ubunge, uwakilishi na udiwani, Mnyika amesema, utaratibu utatangazwa baadaye.
Leave a comment