MICHUANO ya Baraza la mashirikisho ya soka Afrika mashariki na kati ‘CECAFA’ kwa vijana chini ya umri wa miaka 20 yatafanyika 22 Novemba 2020, ambayo yatafanyika nchini Tanzania huku nchi tisa zikithibitisha kushiriki mashindano hayo. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Michuano hiyo itaanza tarehe 22 Novemba hadi 2 Desemba mwaka huu itachezwa kwenye mkoa ya Arusha na kwenye mji wa Karatu huku timu zikiwa kwenye makundi matatu.
Akitoa taarifa hiyo kwa waandishi wa Habari leo tarehe 17 Novemba, 2020, Rais wa CECAFA, Wallace Karia alisema kuwa michuano hiyo ilipaswa kufanyika Sudan ila hali ya ugonjwa wa Covid-19 bado haijatengemaa na mashindano hayo sasa yatafanyika Tanzania katika vituo viwili kwa mikoa ya Arusha na Karatu.
“Sudan walikuwa wenyeji walionesha kule kwa kuwa hali haijatengemaa na ndiyo maana timu yao ipo hapa nchini ikijiandaa, sasa mashindano haya yatafanyika Tanzania na kwa mara ya kwanza tutafanyia mkoa wa Arusha,” alisema Karia.
Kiongozi huyo aliongezea kuwa kwa kawaida mashindano haya yalipaswa kushirikisha timu 12 ila zitakazoshiriki ni timu tisa na yatakwenda mpaka tarehe 2 Decemba, 2020.
“Tutakuwa na timu za Tanzania, Somalia, Djibuti, Kenya, Uganda, Ethiopia, Sudan Kusini na Burundi, ila timu mbili za Rwanda na Elitrea hazitoshiriki kutokana na changamoto za ugonjwa wa Covid-19,” aliongezea Karia.
Michuano hiyo ambayo itakuwa chini ya uangalizi wa Shirikisho la Afrika Afrika ‘CAF’ kwa kuwa itatumika kama sehemu ya michezo ya kufuzu kwa michuano ya vijana ya AFCON kwa timu za Ukanda wa CECAFA.
Kwa upande wa waandaji wa michuano hiyo ambayo ni Tanzania kupitia kwa katibu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Wilfred Kidao alisema kuwa maandalizi yote yapo vizuri na kila timu mpaka sasa imeshapewa kiwanja cha mazoezi na timu ya wataalamu kutoka CAF inatarajia kufika hivi karibuni.
“Mwaka huu kabla ya timu haijafika nchini tumeshavipatia viwanja vya mazoezi na kituo cha Arusha kitakuwa na timu sita ambazo zipo kwenye makundi ya B na C, timu ya Taifa ya Tanzania itakuwepo mjini Karatu ambapo kutakuwa na timu za kundi A,” alisema Kidao.
Leave a comment