RAIS wa Zanzibar,Dk. Hussein Mwinyi ameagiza watu waliohusika katika ubadhirifu wa fedha za umma, uliofichuliwa kwenye Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali visiwani humo (CAG), wachukuliwe hatua. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).
Rais Mwinyi ametoa maagizo hayo leo Jumapili tarehe 23 Mei 2021, baada ya kupokea ripoti ya ukaguzi kwa mwaka wa fedha wa 2019/2020, iliyowasilishwa kwake na Kaimu CAG, Dk. Othman Abbas Ally, Ikulu visiwani Zanzibar.
Katika ripoti hiyo ya CAG Zanzibar, ilifichua ubadhirifu wa fedha za umma katika baadhi ya wizara na taasisi, huku baadhi ya watendaji wake wakigoma kutoa ushirikiano kwa mkaguzi huyo wa hesabu za serikali.
Kufuatia changamoto hiyo, Rais Mwinyi ameagiza watendaji wote waliokwamisha ukaguzi huo, waanze kutoa ushirikiano kuanzia kesho Jumatatu tarehe 24 Mei mwaka huu.
“Imenipa sonono kusikia wafanyakazi wa Serikali wanapofikia kiwango cha kumzuia CAG kufanya wajibu wake, huku ni kukiuka katiba. Naagiza akaendelee pale aliposimamishwa, kuanzia kesho wahusika wote watoe ushirikiano. Nisisikie tena kwamba fulani kazuia kaguzi,” amesema Rais Mwinyi.
Rais Mwinyi amesisitiza “Waliokuwa hawapo labda mtu yuko likizo au ashastaafu, kwenye hili arudi atoe maelezo kwa mkaguzi mkuu. CAG ameeleza pale aliposimamishwa asiendelee alibaini Sh. 5 Bil. hazina maelezo, akimaliza hatujui bilioni ngapi zitapotea.”
Mwenyekiti huyo wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar, amewaagiza mawaziri na makatibu wakuu wa wizara, kuhakikisha dosari zilizojitokea katika ukaguzi huo, zisijirudie tena.
“Hatuwezi sema tumepokea yamekwisha hata kidogo, tumepokea tuchukue hatua, ripoti ya mwakani tukija kuipokea kusiwe na karoso hizi, zikiwepo maana yake tunashindwa kutekeleza wajibu wetu nitakuwa wa kwanza kutokubali kuonekana nashindwa kutimzia majukumu yangu,” amesema Rais Mwinyi.
Rais Mwinyi amewataka mawaziri hao kutowafumbia macho watendaji wao watakaobainika kuhusika katika vitendo vya ubadhirifu wa fedha.
“Sote tuliopo hapa, mawaziri na makatibu wakuu ndiyo wasimamizi wakuu kuna mashirika na taasisi ambazo ziko chini yenu, hatuwezi sema kafanya fulani mimi sihusiki hata kidogo, kama uwajibikaji lazima uanze juu hadi chini,”amesema Rais Mwinyi na kuongeza:
“ Nitafurahi kusikia fulani nimemfukuza au nimemsimamisha au nakuletea rais uchukue hatua kwa sababu ya hili, lakini kusikia fulani kafanya makosa yuko chini ya taasisi yako hata kusema hujasema huwezi kuepuka lawama.”
Leave a comment