BARAZA la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGO’s), nchini Tanzania- NACONGO, limeomba kufanya mazungumzo na Rais Samia Suluhu Hassan, ili kutafuta suluhu ya changamoto zinazozikabili mashirika hayo. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
Ombi hilo limetolewa jana tarehe 9 Julai 2021, jijini Dodoma na Mwenyekiti wa NACONGO, Lilian Joseph Badi, baada ya kuchaguliwa kushika wadhifa huo, kupitia uchaguzi wa baraza hilo uliofanyika juzi jijini humo.
Lilian aliomba kukutana na Rais Samia, ili wajadili namna ya kuweka mikakati ya ushirkiano baina ya mashirika hayo na Serikali yake, hususan katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya wananchi.
Aidha, Lilian alisema baraza hilo litahakikisha linaleta umoja kati ya NGO’s, wadau na Serikali, ili kuhakikisha utekelezaji wa mipango mikakati iliyowekwa na Serikali katika kuwaletea wananchi maendeleo, inafanikiwa.
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Idara Kuu ya Maendeleo Jamii, Patrick Golwike, alilitaka baraza hilo kufanya kazi kwa kuzingatia sheria za nchi.
Ili kuisaidia Serikali katika kutatua changamoto zinazowakabili wananchi, kwenye kujiletea maendeleo.
Leave a comment