WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa ameonya uwepo wa aina nyingine ya bangi yenye kiasi kikubwa cha kilevi inayofahamika kwa jina la ‘Cha Arusha’ pamoja na ‘Skanka’ ambayo amesema ina kiasi kikubwa cha sumu kinachosababisha vijana wengi wanaotumia kuwa vichaa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kilimanjaro … (endelea).
Akizungumza katika uzinduzi wa mbio za Mwenge wa Uhuru leo Jumanne mjini Moshi mkoani Kilimanjaro, Majaliwa amesema mbio hizo za mwaka huu zitaendelea kuhamasisha jamii kusitisha kilimo hicho haramu cha bangi, mirungi pamoja na biashara na matumizi yenyewe.
“Aina hii ya bangi yenye sumu nyingi huchanganywa kwenye sigara lakini ukishaitumia, watumiaji wanabadilika na kuwa vichaa.
“Ni wakati mzuri sasa vijana ambao mmekuwa mkitumika na kutumia Cha Arusha na Skanka muache ili kunusuru maisha yenu. Vijana mnahitajika katika taifa hili, ndio mtakaolijenga… Cha Arusha na Skanka vitawapoteza,” amesema.
Amesema jambo la kusikitisha ni kuwa vijana wamekuwa wakitumia bidhaa hizo huku wengine wakifahamu uwepo bangi hiyo mpya na wengine kutofahamu hali inayowafanya kuwa waraibu wa bangi.
Ameaema idadi kubwa ya waathirika wa matumizi hayo ya dawa za kulevya ni watoto na vijana wenye umri wa miaka 13 hadi 24.
“Serikali imeongeza kasi ya kutokomeza uzalishaji, matumizi na biashara dawa hizi za kulevya. Mikoa inayoongoza kwa kilimo cha bangi na mirungi ni pamoja na Mara, Morogoro, Arusha, Pwani, Kagera na Mwanza. Nitoe onyo kwa wakulima wa bangi kuwa hatua kali zitachukuliwa pindi watakapokamatwa.
Leave a comment